SERIKALI imetenga bilioni 13 kwa ajili ya kujenga minara ya mawasiliano na usalama 44 mkoani Kagera ambayo itawezesha vijiji 66 kupata mawasiliano ya uhakika.
Akizungumza mkoani Kagera, Naibu Waziri wa Habari na Tekinolojia, Mhandisi Kundo Mathew alisema mradi huo utakamilika ndani ya miezi tisa hata hivyo mikataba ilisainiwa Mei mwaka huu.
Alisema Kagera wanakabiria na changamoto ya kuingiliana na mtandao wa nchi nyingine na maeneo mengi kukosa mtandao hivyo ujenzi wa minara hiyo utakuwa uchumi wao kupitia mawasiliano imara na kupitia inteneti.
Alisema kuwa serikali inadhamiria ifikapo mwaka 2025 Watanzania asilimia 80 watumie Intenet hivyo minara yote inayojengwa nchini kwa sasa inauhakika wa kufanya kazi ngazi ya vijiji kuanzia kasi ya 2G-5G.
Aidha alifanya ukaguzi wa minara katika kijiji Cha Bugorora na Kanazi minara ya mawasiliano ambayo imekamilika kupitia usimamizi wa makampuni ya simu ya Vodacom na Tigo ambapo amepongeza ukamilikaji wa ujenzi wa minara hiyo huku wananchi wakiendelea kufurahia uwepo wa mtandao katika vijiji vyao.
Alitoa wito kwa wasimamizi wa mfuko wa mawasiliano kwa wote UCSAF kuhakikisha wanawasimamia wakandarasi ili waweze kumaliza miradi Yao kwa wakati bila kukiuka mikataba waliyosaini.
Awali Katibu Tawala Mkoa wa Kagera, Toba Nguvilla alimwambia naibu waziri huyo kuwa ukosefu wa mawasiliano katika vituo vya mipaka ya Mkoa wa Kagera na maeneo ya visiwa kunapelekea changamoto ya kutopata mapato kwani zoezi la kukata vibali vya kibiashara pamoja na taarifa uchelewa kutokana na Vituo vingi vya mipakani kusoma mtandao wa nchi nyingine.
Alipongeza serikali kwa kuwekeza katika kuimarisha mawasiliano, usalama na kujikita katika maswala ya Kidgital kwani ongezeko la watumiaji wa mtandao likiwa kubwa hata serikali itaongeza mapato na hali ya usalama itaendelea kuimarika kwa mikoa ya pembezoni.