Sh bilioni 27 kuboresha mazingira ya elimu TIA

TAASISI ya Uhasibu Tanzania (TIA), imetengewa kiasi cha Sh bilioni 27.3 kutoka kwenye Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET), zitakazotumika kuboresha mazingira ya kusomea na kujifunza kwa wanafunzi kwa lengo la kutoa wahitimu watakaoweza  kujiajiri na kuajiri wengine kulingana na soko la ajira.

Mratibu wa mradi wa HEET kutoka Taasisi hiyo, Oyombe Simba alisema mjini Morogoro kwenye kikao kazi kilichowakutanisha wadau na watumishi wa Taasisi kupitia  mchakato wa kuboresha  mitaala itakayoenda na matakwa ya utekelezaji wa mradi huo.

Advertisement

Simba ,alisema  katika utekelezaji wa mradi huo kuna maeneo  saba ya kutekelezwa ukiwemo ujenzi wa  hosteli katika kampasi ya Mwanza , kujenga  jengo  la taaluma kampasi ya Singida  na  kuboresha  wa mitaala  itakayompa zaidi mwanafunzi elimu ujuzi anapomaliza  chuo aweza kujiajiri ama kuajiri wengine .

Alisema, mradi huo umejikita katika maeneo saba na moja walo ni  kuboresha mitaala ili iendane na soko la ajira  kwa lengo la  kutoa wahitimu wenye kuweza  kujiajiri  na kuajiri wenzao

Mratibu huyo wa HEET kutoka Taasisi hiyo alisema kuwa, katika kipengere cha uboreshaji wa mitaala kiasi cha  takribani sh milioni 250 kinatarajiwa kutumika.

Simba alisema mchakato wa maboresho ya mitaala  imeshaanza kwa kufanya  kikao cha  kwanza cha wadau kupitia mitaala na kufanya maboresho na kupeana uelewa kwa kile kitakachofanyika.

“Katika mchakato huo kutakuwa na maboresho ya  mitaala , kutengeneza mitaala mingine mipya  na huu ni  mchakato ambao kidogo unachukua muda  na tunatarajia kadiri ya miezi sita  hadi nane ijayo  tutakuwa tumetimiza maboresha mitaala na kuja na mingine ambayo itawezesha  kukudhi  matakwa ya mradi “ alisema Simba

Kwa upande wake Makamu Mkuu wa Chuo Uhasibu anayesimamia Taaluma , Utafiti na Ushauri wa Kitaalam wa TIA , Dk Momole Kasambala alisema kuwa, licha ya  kuboresha mitaala , mradi huo una lenga uboreshaji wa mifumo (ICT) na Tehama.

“ Tunataka kuchopeka vitu vingi  kwenye mtaala yakiwemo masuala ya mifumo au Tehama ili kila  taaluma inayotolewa  na Taasisi yetu umwezeshe  mwanafunzi kujua kila kitu kitaaluma na  mengineyo” alisema Dk Kasambala

Dk Kasambala alisema ,mitaala hiyo itakuwa shirikishi kwa watu wenye ulamavu , wanafunzi wenye kunyonyesha na ikijizngatia  kijinsia  na itakuwa na viwango vya  kimataifa  kuwawezesha mwanafunzi  kutoka nje ya Tanzania na kujiunga kusoma moja kwa moja  kwenye Taasisi hiyo.

“ Lengo kubwa ni kuboresha na kuweka mitaala iwe ni ya kimataifa , ijali  wenye mahitaji maalum na ichukue masuala na jinsia na kuhusisha program  za chuo kupatikana kwenye mtandao au kuchanganya darasani na kwenye mtandao “ alisema Dk Kasambala

Dk Kasambala alisema ,Taasisi hiyo inapitia  na kuandaa  mitaala sita ambapo mitatu ni kwa ajili ya wanafunzi wa shahada ya Uzamili na mitatu mingine ni kwa ajili ya wanafunzi wa shahada ya kwanza.

Kwa mujibu wa Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia ,Profesa Adolf Mkenda  ,Septemba 13, 2022  wakati wa  utaji saini makubaliano ya utekelezaji wa mradi huo ambao unaofadhiliwa na Benki ya Dunia kuwa imetoa  mkopo wa masharti nafuu wa fedha takribani Sh trilioni moja  kwa ajili ya kuleta mageuzi katika utoaji wa elimu juu nchini.

Mradi wa HEET unakwenda kujenga miundombinu, kununua vifaa wezeshi vya kujifunzia na kusomesha wahadhiri ambapo Vyuo Vikuu vya umma 14, Taasisi Tatu zilizo chini ya Wizara zinazosimamia elimu ya juu na Taasisi Tano zilizo chini ya Wizara ya Fedha watanufaika.

2 comments

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *