CHUO Kikuu cha Mtakatifu Augustine Tanzania (SAUT) kimefuta shahada za wahitimu 162 wa fani ya udaktari waliohitimu Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi cha Mtakatifu Francis (SFUCHAS) kuanzia mwaka 2015 hadi 2019.
Mwenyekiti wa Baraza la Seneti la chuo hicho Balozi Profesa Costa Mahalu ameeleza kuwa shahada hizo zimefutwa kwa kuwa wahusika walikataa kurejesha nakala za matokeo ya taaluma hiyo waliyopewa bila chuo kufahamu na pia bila idhini ya Baraza la Seneti la SAUT.
Taarifa ya chuo hicho kwa umma imeeleza kuwa uamuzi huo ulifikiwa katika kikao cha 54 cha Baraza la Seneti la SAUT kilichofanyika katika kampasi ya chuo hicho Mwanza Februari 25, mwaka huu.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo wahitimu hao pamoja na kutakiwa kurudisha nakala za matokeo hayo, walikaidi agizo hilo kwa makusudi hali iliyosababisha chuo kuchukua hatua hizo.
“Kulingana na Kifungu cha 47 (1) na (2) cha Sheria Namba 7 ya vyuo vikuu ya mwaka 2005 ikisomwa pamoja na ibara ya 6(3) (II), 7, 8 na kifungu cha 29 (1) cha tamko la SAUT kwenye tangazo namba 580 la mwaka 2020 chuo kimefuta shahada zilizotolewa kwa wahitimu 162 wa shahada za udaktari (SFUCHAS) waliohitimu kutoka mwaka 2015 hadi 2019,” ilieleza taarifa hiyo ya Profesa Mahalu.