DAR ES SALAAM: KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria imepanga kupokea maoni ya wadau kuhusu Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali Namba Mbili wa Mwaka 2023 ambao pamoja na mambo mengine unapendekeza kurekebisha sheria ya Mamlaka ya Nchi Kuhusiana na Umiliki wa Mali na Rasilimali Asilia Sura ya 449.
Pia unapendekeza marekebisho ya Sheria ya Mapitio na Majadiliano Kuhusu Masharti Hasi Katika Mikataba ya Mali na Rasilimali Asilia.
Taarifa ya Katibu wa Bunge, Nenelwa Mwihambi imeeleza kuwa muswada huo utajadiliwa na kamati hiyo. “Katika kutekeleza jukumu hilo, kwa mujibu wa Kanuni ya 97(2) ya Kanuni za Kudumu za Bunge, Toleo la Februari, 2023, Kamati itasikiliza na kupokea maoni ya wadau siku ya Jumatano Agosti 16, 2023 saa 4:00 asubuhi katika Ukumbi wa Frank Mfundo, Ghorofa ya tano Jengo la Utawala, Ofisi ya Bunge jijini Dodoma,” alisema.
Kwa mujibu wa muswada huo, sheria hizo zinarekebishwa ili kuhakikisha utekelezaji wake hauathiri utendaji wa maeneo ya bandari, bandari za nchi kavu na bandari za maeneo ya maziwa nchini. Pia sheria hizo zinarekebishwa kuziwezesha bandari katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kufikia viwango vya kimataifa vya kiutendaji na kuvutia nchi nyingi zaidi na shehena za mizigo kutumia bandari za hapa nchini.
Comments are closed.