Sheria zinazoratibu uhuru wa habari ziboreshwe

Sheria zinazoratibu uhuru wa habari ziboreshwe

KIKOSI Kazi cha kuratibu maoni ya wadau wa demokrasia ya vyama vingi kimependekeza sheria zinazoratibu uhuru wa habari ziboreshwe kukuza uhuru wa habari na demokrasia nchini.

Vilevile kimependekeza wanahabari wenyewe waunde chombo cha kusimamia maadili ya wanahabari na vyombo vya habari.

Hayo yamebainishwa na Mwenyekiti wa Kikosi Kazi hicho, Profesa Rwekaza Mukandala, wakati wa kukabidhi ripoti yao kwa Rais Samia Suluhu Hassan, Ikulu Dar es Salaam jana.

Advertisement

Kwa mujibu wa Profesa Mukandala, baadhi ya sheria zinapaswa kubadilishwa kuondoa pia mamlaka ya Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo kufungia vyombo vya habari bila kuwapo kwa mchakato wa wazi wa kuviwajibisha.

Profesa Mukandala alitaka uwepo utaratibu wa kusimamia utekelezaji wa sheria husika vyombo vya habari vya umma vitoe fursa sawa ya kutangaza habari za wagombea na vyama vya siasa wakati wa uchaguzi bila upendeleo.

“Ziandaliwe kanuni zitakazoeleza vyombo vya habari kuheshimu maadili ya taaluma ya uandishi wa habari ikiwemo mwanahabari kuhakikisha anahakiki habari aliyoipata kutoka pande zinazohusika kabla ya kuitangaza au kuichapisha habari husika,” alisema Profesa Mukandala.