SERIKALI imetenga shilingi bilioni 752 kwa ajili ya kutekeleza shughuli mbalimbali kupitia Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET).
Akizungumza leo Septemba 23,2022 wakati akiahirisha Bunge la 12 mjini Dodoma, Waziri Mkuu Kassim amesema shughuli zitakazotekelezwa kupitia mradi huo ujenzi wa miundombinu mipya na kukarabati iliyopo ikiwemo kumbi za mihadhara na madarasa 130, maabara na karakana 108, mabweni 34 na ofisi 23.
Amesema kupitia mradi huo Serikali inatarajia kukarabati na kuboresha miundombinu ya mashamba darasa na vituo atamizi 10 pamoja na kuweka vifaa vya kisasa vya TEHAMA katika vyuo vikuu na taasisi.
“Serikali imepanga kujenga kampasi mpya 14 katika mikoa ya Dodoma, Kagera, Katavi, Kigoma, Lindi, Manyara, Mwanza, Rukwa, Ruvuma, Simiyu, Singida, Shinyanga, Tabora na Tanga.” Amesema
Aidha, amesema Serikali imepanga kujenga Chuo Kikuu cha kisasa cha TEHAMA mkoani Dodoma na Chuo Kikuu cha Kilimo na Teknolojia cha Mwalimu Julius Nyerere mkoani Mara pamoja na kusomesha wahadhiri katika shahada za uzamivu na shahada za umahiri ili kuwajengea uwezo katika fani .