SHULE ya Sekondari Mazwi iliyopo mkoani Rukwa, imepongezwa kwa kuandika insha mbalimbali zinazoelimisha jamii kuhusu athari za dawa za kulevya, kupinga ukatili wa kingono na madhara ya matumizi hasi ya mtandao.
Pongezi hizo zimetolewa na Naibu Katibu Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania (LRCT) na Mkuu wa kitengo Cha Elimu ya Sheria kwa Umma, Zainab Chanzi, baada ya kupokea nakala tisa za insha zilizopita mchujo wa kwanza, kisha kuzichuja na kupata washindi watatu kati ya tisa.
Amewataja wanafunzi waliofanya vizuri kuwa ni Lucy Ally aliyeandika insha inayohusu athari za dawa za kulevya Katika jamii, Shabani Mrisho aliyeshinda insha ya ukatili wa kingono na Neema Sigfrid Kapaya, ambapo kila mmoja amezwadiwa Sh 30,000.
Amesema uandishi wa insha ni matokeo ya elimu ya sheria iliyotolewa hivi karibuni katika mkoa wa Rukwa, ambapo tume ilitoa elimu ya makosa dhidi ya maadili, sheria ya kudhibiti na kupambana na dawa za kulevya, sheria ya makosa ya kimtandao na sheria ya utakasishaji wa fedha haramu.
Naye Mkuu wa shule hiyo, Mwalimu Mwaibingila amesema baada ya kupata elimu hiyo wamejipanga kuwa mabalozi wa kupinga matumizi ya dawa za kulevya, ukatili wa kingono pamoja na makosa ya kimtandao kwa kuunda klabu mbalimbali.