Simba wapo kamili kuivaa Raja

NAHODHA wa Simba, John Bocco amesema pamoja na uchovu wa safari kuwasumbua, lakini watacheza kwa nguvu kuhakikisha wanaibuka na ushindi.
Akizungumza kuelekea mcheo huo, nahodha huyo ameeleza kuwa anatambua haitokuwa rahisi, lakini kwa namna walivyojipanga dhamira yao ni kulipa kisasi, ili kumaliza mechi za hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika kwa heshima.
“Ni mchezo mgumu hata Raja Casablanca wenyeji wanalitambua hilo, tumekuja huku lengo tunataka kuonesha ukubwa wa Simba siyo tunapocheza nyumbani hata ugenini, ndio mana tumejipanga kucheza kwa nguvu, ili kupata ushindi,” amesema Bocco.
Simba inatarajia kushuka katika dimba la Mohamed V leo saa 4 usiku kwa saa za Morocco, ambapo kwa Tanzania itakuwa ni saa 7 usiku na matokeo ya mchezo huo hayatoathiri msimamo wa kundi hilo linaloongozwa na Raja Casablanca wenye pointi 13 wakifuatiwa na Simba wenye pointi 9.