Sudan Kusini kujenga bandari Djibouti
SUDAN Kusini imenunua kipande cha ardhi nchini Djibouti kwa ajili ya ujenzi wa bandari.
Hii ni sehemu ya juhudi zake kutafuta njia mbadala ya Bandari ya Mombasa.
Imenunua ekari tatu za ardhi katika Bandari ya Djibouti kwa ajili ya ujenzi wa kituo kitakachoshughulikia uagizaji na usafirishaji wa bidhaa zake huku ikijaribu kupunguza utegemezi wake kwa Bandari ya Mombasa.
Hatua hii inakuja miezi miwili tu baada ya Chama cha Wafanyabiashara nchini hapa kusema kuwa kitahamisha shehena yake kwenye Bandari ya Djibouti iliyoutaja kuwa rahisi kwao,
Waziri wa Petroli, Puot Kang Chol, alinukuliwa akisema: “Tumekuwa tukitumia Bandari ya Sudan na Mombasa pekee, lakini hivi majuzi, tumeamua kwenda Djibouti na hivi ninavyozungumza nanyi, tuna ardhi nchini Djibouti.”
Alisema ardhi hiyo ilinunuliwa na Wizara ya Petroli kwa madhumuni ya kusafirisha mafuta ghafi ya nchi na kuyatumia kwenye bidhaa zinazoagizwa kutoka nje.
Iwapo itatekelezwa, hatua hiyo itaiathiri Bandari ya Mombasa hasa ikizingatiwa kuwa, Sudan Kusini ni moja ya wateja wakubwa wa Kenya.
Mombasa imekuwa njia kuu kwa shehena zote zinazoingia nchini.