TADB yatoa mkopo wa sh bilioni 317

BENKI ya Maendeleo ya Kilimo ( TADB) imetoa mkopo wa sh bilioni 317 tangu Rais Samia Suluhu Hassan aingie madarakani.

Hayo yamesemwa leo Julai 6 ,2023 na Mkurugenzi wa Benki hiyo Frank Nyabundege katika Uzinduzi wa Ofisi ya Benki hiyo Kanda ya Kusini ambako Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ndio mgeni rasmi.

Amesema, mikopo hiyo imetolewa kwa wakulima, wafugaji na wavuvi na kufanya mizania ya mikopo kukua na kufikia kiasi cha sh bilioni 317 hadi kufikia June 2023.

Advertisement

” Ili ni ongezeko la asilimia 164 kwa kipindi cha miaka miwili.” Amesema

Amesema, pia benki hiyo imekuza mizania yake na kufikia kiasi cha sh bilioni 490 mwezi June, 2023 kutoka sh bilioni 362 kwa kipindi hicho.

Aidha, amesema wakati serikali ya awamu ya sita inaingia madarakani TADB ilikua na ofisi katika Kanda tatu lakini sasa hivi zimeongezeka nne na kuifanya TADB kuwa na ofisi katika Kanda saba ambazo ni Mbeya, Mwanza, Dodoma, Arusha, Dar es Salaam, Tabora na ya Mtwara ambayo imezinduliwa leo.

Nyabundege, amesema tayari TADB imeshapata Ofisi Zanzibar na kwamba kwa sasa wanasubiri vibali kutoka Benki Kuu (BOT) ili iweze kufungua ofisi hiyo.

Akizungumzia Ofisi ya Kanda ya Kusini Mkurugenzi huyo wa TADB amesema Mtwara inachangia asilimia 2.7 ya pato la taifa na pato la wastani la mwananchi ni sh milioni 2.

Amesema, sekta ya kilimo imeajiri asilimia 90 ya idadi ya nguvu kazi ya watu wa Mtwara.

Aidha, amesema pamoja na kuizindua ofisi hiyo leo, tawi hilo lilianza kufanya kazi tangu Agosti 2022 ambapo hadi kufikia June 2023 wamefikia wakulima 2,831 katika Mikoa yote ya Kanda hiyo ya Kusini.

“Katika kipindi hicho benki ilitoa mikopo yenye thamani sh bilioni 7.329 katika hiyo sh bilioni 356 zilikopeshwa kwa wakulima 2,831 katika mikoa yote ya Kanda ya Kusini.” Amesema

Akifafanua amesema katika mikopo hiyo,wakulima wa zao la mahindi walikopeshwa sh bilioni 3.56 , wakulima wa zao la korosho walikopeshwa sh bilioni 2.71 wakati sh milioni 500 zilitolewa kwa ajili ya unenepeshaji wa mifugo kama vile mbuzi na ng’ombe.

Amesema sh milioni 300 zilielekezwa kwenye ufugaji wa kuku, huku sh milioni 249.2 zilikopeshwa kwenye zao la kahawa.

 

2 comments

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *