Taifa Gas kuanza kuzalisha umeme Zambia

ZAMBIA: KAMPUNI ya Taifa Group, imeingia imeingia mkataba wa kuzalisha umeme kwa kutumia gesi nchini Zambia.

Mkataba huo umeingiwa na Mfanyabiashara maarufu Rostam Azizi chini ya kampuni yake tanzu ya Taifa Gas na Kampuni ya Delta Marimba ya nchini Zambia.

Rostam, amewekeza kiasi cha awali cha Dola milioni 100 katika uwekezaji huo kwa kushirikiana na kampuni hiyo ya Delta Marimba.

Advertisement

Akizungumzia mkataba huo, Rostam amesema mtambo wa kwanza wa kuzalisha umeme kwa kutumia gesi utajengwa katika eneo la Kasama nchini Zambia.

“Uwekezaji tuliofanya umemfurahisha Rais wa Zambia, Hakainde Hichilema, amehaidi serikali yake kutupa ushirikiano mkubwa tulipomtembelea Ikulu Zambia. ” Amesema

Aidha, amesema Rais Hichelema amesema ubia wa aina hiyo ni moja ya njia nzuri za kuhakikisha Afrika inaondokana na utegemezi kutoka nchi za mataifa yaliyoendelea.

Amesema, ubia wa aina hiyo utaipatia Afrika nguvu ya kutumia rasimali zake kwa ajili ya uzalishaji badala ya rasilimali hizo kuzinufaisha nchi nyingine.

Rais Hichelema amesema hivi sasa nchi yake inaangalia namna ya kuongeza uzalishaji umeme kwa kutumia njia mbadala wa maji kutokana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

“Kwa hiyo kuja kwa Taifa Marimba na kuwekeza katika uzalishaji umeme kwa kutumia gesi kunaendana na mtazamo wetu, Tunaziunga mkono juhudi hizi na ningewahimiza mfanye haraka kukamilisha uwekezaji huu,” amesema.

Kwa upande wa Rostam, uwekezaji wa awali unalenga katika kubadilisha mitambo inayotumia dizeli ili iweze kuzalisha umeme kwa kutumia gesi lakini hapo baadaye uwekezaji utaelekezwa pia kuzalisha umeme kwa kutumia nguvu za upepo na jua.

“Pia tutawekeza katika maeneo mengi nje ya uzalishaji umeme kwani tumeona Zambia kuna fursa nyingi za uwekezaji,” amesema.

Amesema, Taifa Marimba imeamua kufanya uwekezaji huo kwa dhamira ya kutaka kudumisha uhusiano wa kindugu na wa muda mrefu baina ya nchi hizo mbili.

“Pia tunafanya hivi tukiamini kuwa ubia baina ya kampuni za Afrika utatupatia nguvu ya kuweza kufanya mambo mengi makubwa sisi wenyewe bila kumuangalia mtu mwingine kutoka nje ya bara letu; ……..

“Tunaamini kuwa kwa kuunganisha nguvu tunaweza kutatua matatizo yetu mengi huku tukihakikisha rasilimali zetu zinatumika kama malighafi hapa nchini badala ya kuwanufaisha watu wengine wa nje,” alisisitiza Rostam.

Zambia inakuwa nchi ya pili kwa Rostan na kampuni yake ya Taifa Gas kuwekeza katika ukanda wa SADC, mapema mwaka huu kampuni hiyo iliingia nchini Knya ambako inajenga kiwanda cha kuchakata gesi ya kupikia jijini Mombasa.

3 comments

Comments are closed.