TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), imesema itasambaza filamu maalum ya kufundisha maadili mema katika shule zote za msingi nchini.
Filamu hiyo iliyozinduliwa leo jijini Dar es Salaam inayofundisha maadili mema kwa watoto ilitengenezwa kupitia mradi wa Tabia Njema Kids Animation unaoitwa Tanjema.
Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi wa TAKUKURU, Mkurugenzi wa Elimu kwa Umma, Joseph Mwaswelo amesema filamu hiyo itasambazwa kupitia klabu za kupinga rushwa zilizopo katika shule mbalimbali nchini.
Amesema pia katika shule hizo kuna klabu za taasisi zingine mfano Mamlaka ya Mapato ,uhamiaji hivyo wote wataongeza nguvu kuhakikisha filamu hiyo itafikia wengi na kuwa na uadilifu.
Mwaswelo amesema TAKUJKURU imepewa jukumu la kuhakikisha Tanzania inaongozwa katika misingi ya utawala bora na kuhakikisha inapambana na kuondoa rushwa nchini.
” Filamu hiyo imeandaliwa kwa ajili ya kuelimisha Watanzania kupitia wanafunzi, ili waweze kuwa na maadili na imeandaliwa kuhakikisha nchi inakuwa na maendeleo yenye ustawi mzuri.
Kwa upande wake Msimamizi wa Mradi, Fredrick Fussi amesema waliandaa filamu hiyo baada ya kuona kuna mmonyoko wa maadili miongoni mwa watoto na vijana hapa nchini.
Amesisitiza kuwa wanaamini kwamba watakapoweza kutengeneza filamu hiyo na wakiweza kuwafundisha watoto maadili wakiwa wadogo, wataweza kuzingatia mambo matatu ambayo ni kutimiza wajibu wao,kuzingatia kutenda haki na kutii sheria za nchi.