TAKUKURU yaanza uchunguzi ujenzi madarasa, mabweni

Kamanda wa Takukuru Morogoro Manyama Tungaraza

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Tanzania ( TAKUKURU), Mkoa wa Morogoro imeanza kazi ya kufuatilia kwa karibu fedha zilizotolewa na serikali kwa ajili ya ujenzi wa  madarasa na mabweni ya wanafunzi watakaoingia kidato cha kwanza mwaka 2023 mkoani humo.

Ufuatiliaji huo wa karibu unalenga kujiridhisha  na kuona iwapo fedha hizo zimetumika kwa lengo lililokusudiwa na ujenzi wake imezingatia viwango vya ubora.

Mkuu wa Takukuru mkoa huo, Manyama Tungaraza amesema hayo kupitia taarifa yake kwa vyombo vya habari  kuhusu  utekelezaji wa majukumu ya Taasisi hiyo  kwa kipindi  cha Julai mwaka  huu hadi Septemba , 2022.

Advertisement

” Niwakumbushe wasimamizi wa miradi hiyo  waweze kutekeleza kwa haraka kama maagizo yaliyotolewa ifikapo  mwezi Januari 2023 , wanafunzi wa kidato cha kwanza waweze kuanza masomo yao “ amesema Tungaraza

Pia amesema Takukuru inaendelea kufualilia matumizi  ya mbolea ya ruzuku zilizotolewa na serikali kwa ajili ya wakulima  mkoani humo.

Tungaraza ametoa rai kwa wote watakaojihusisha na udanganyifu wowote kwa ajili ya kuhujumu mbolea ya ruzuku , watachukuliwa hatua kali.

Amesema kipindi cha Oktoba hadi Desemba 2022, Takukuru imeweka mikakati ya kufanya ufuatiliaji wa mara kwa mara katika miradi inayotekelezwa  mkoani humo kwa kushiriana na taasisi zilizopewa jukumu la kuteleleza miradi hiyo.

Amezitaja baadhi ya taasisi hizo ni pamoja na  Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) , Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA), Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Morogoro (MORUWASA) na halmashauri za wilaya zilizilizopo  mkoani  huo.

Takukuru imefanya mawasiliano na  Meneja wa TARURA  na RUWASA ambao wameafiki kufanya ukaguzi wa miradi kwa kushirikiana  na kwamba mawasiliano yatafanyika kwa taasisi zilizobaki  kwa maana ya Tanroads , Moruwasa na halmashauri za wilaya za mkoa huu” amesema  Tungaraza.

Amesema jukumu lingine ni kufuatilia kwa ukaribu mifumo ya ukusanyaji wa mapato katika halmashauri ili kudhibiti upotevu wa fedha za umma  na kuendelea  kutoa elimu ya mapambano dhidi ya rushwa kwa jamii kupitia mpango wa Takukuru inayotembea  , pamoja na mikutano ya hadhara .

Takukuru pia inaendelea na  uchunguzi wa miradi mitatu ya sekta ya afya  ambao uko katika hatua mbalimbali inayohusu  miradi  hiyo  ambayo ilikataliwa  kuwekewa mawe ya msingi  na Mbio za Mwenge wa Uhuru  2022 kwa maelekezo kutoka kwa Kiongozi wa Mbio za Mwenge  ya kufanya uchunguzi  ili kubaini thamani halisi ya fedha za miradi hiyo.

Miradi hiyo  ni ujenzi wa kituo cha Afya Itete wilaya ya Malinyi wenye thamani ya Sh milioni 345.2 , mradi wa kituo cha afya Igima wilaya ya Kilombero wenye thamani ya Sh milioni 500 na mradi wa jengo la wagonjwa wa dharura Hospitali ya wilaya ya  Gairo wenye thamani ya Sh milioni 300 .

Add a comment

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *