KATAVI; Taasisi ya kuzuia na kupambana na Rushwa (Takukuru) Mkoa wa Katavi, imefanya uchambuzi wa mfumo kwenye Halmashauri za Mpanda, Nsimbo, Mlele na Tanganyika kwa lengo la kubaini mianya ya rushwa.
–
Akitoa taarifa kwa umma mbele ya waandishi wa habari, Kaimu Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Katavi, Stuart Kiondo amesema moja ya jambo walilolibaini ni uwepo wa njia mbili tofauti za ukusanyaji wa kodi ya zuio katika halmashauri, badala ya mfumo mmoja wa ukusanyaji na pia mamlaka ya mapato kukosa uwezo wa kutambua kiasi cha kodi ya zuio inachopaswa kukusanya.
Pia imebaini uwepo wa baadhi ya wakusanyaji wa kodi ya zuio kutokuwa na weledi wa kutosha juu ya matumizi ya teknolojia ya Habari na Mawasiliano (Tehama) na mifumo sanjari na baadhi ya walipwaji kutowasilisha stakabadhi za mashine au kuwasilisha kwa kuchelewa.
Amesema kutokana na kasoro hizo yamefikiwa makubaliano kuwa mifumo yote ya ukusanyaji wa kodi ya zuio iunganishwe, ili kuhakikisha kuwa kila fedha inayotolewa kwa mlipwaji inajulikana TRA na kodi yake ya zuio inakuwa wazi, ili kuzuia uvujaji wa mapato ya serikali .
Pia imeshauri kutolewa mafunzo kwa wasimamizi wote wa miradi wa ngazi ya chini, ili kuwajengea uwezo wa kukusanya kodi ya zuio kwa weledi.