TAASISI ya Masai Festival, imeandaa tamasha lenye kujumuisha jamii ya Wamasai, lengo likiwa ni kupongeza juhudi zinazofanywa na Rais Samia Suluhu Hassan za kukuza utalii nchini na kuongeza mapato.
Pia imesema ipo tayari kushiriki kutafuta vazi maalum la Taifa, jambo litakaloongeza wigo wa Tanzania kujitangaza kitalii na kiutamaduni zaidi.
Mwanzilishi wa taasisi hiyo, Said Rukemo, amesema hayo katika maonesho ya sita ya Kimataifa ya Utalii ya Swahili (SITE) yanayojumuisha wanunuzi na wauzaji mbalimbali wa bidhaa za kitalii nchini.
Kuhusu tamasha la Masai, amesema limeitwa la Masai Kwa sababu ni kabila pekee nchini lililodumisha mila na tamaduni na limekuwa utambulisho mzuri ndani na nje ya nchi.