Tamisemi yaomba kuidhinishiwa Sh trilioni 9.1

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Angellah Kairuki ameliomba Bunge likubali kuidhinisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 kiasi cha Shilingi Trilioni Tisa Bilioni Mia Moja Arobaini na Nne Milioni Ishirini na Moja na Mia Sita Tisini na Tisa Elfu (Tsh. 9,144,021,699,000).
Akiwasilisha bajeti ya ofisi hiyo leo Aprili 14, 2023 Kairuki amesema, upande wa Sekta ya Elimu ya Msingi na Sekondari maeneo yaliyopewa kipaumbele elimu bila ada kwa Shule za Msingi na Sekondari ambapo Shilingi Bilioni 399.64 zimetengwa.
“Kati ya fedha hizo Shilingi Bilioni 157.79 zimetengwa kwa ajili ya Shule za Msingi na Shilingi Bilioni 241.85 zimetengwa kwa ajili ya Shule za Sekondari.”Amesema na kuongeza
“Bajeti hiyo ni sawa na ongezeko la Shilingi Bilioni 53.15 sawa na asilimia 15.34 ikilinganishwa na bajeti ya Shilingi Bilioni 346.49 iliyoidhinishwa katika Mwaka wa Fedha wa 2022/23, ongezeko hili linatokana na Wanafunzi wa kidato cha tano na sita kujumuishwa katika Mpango wa Elimu Bila Ada”