SERIKALI ya Tanzania na Canada zimeingia makubaliano ya ushirikiano ya kuboresha afya za vijana balehe nchini Tanzania kupitia mradi wa shirika la Nutrition International.
Wakizungumza leo Julai 20, 2023 jijini Dodoma Waziri wa Maendeleo ya Kimataifa wa Canada, Harjit Sajjan na Waziri wa Afya wa Tanzania, Ummy Mwalimu, wametangaza mradi mpya unaoongozwa na tasisisi hiyo.
Katika hatua hiyo serikali ya Canada imetoa fedha kiasi cha Dolaza Marekani milioni 15 kwa ajili ya Kujenga Haki za Kuboresha Afya ya Wasichana Tanzania.
Mradi huo ni wa miaka saba ambao utatekelezwa mkoani Tabora na Shirika la Nutrition International kwa kushirikiana na washirika wake, ambao ni Engender Health na Young and Alive Initiative, pamoja na mradi huu ulitangazwa pamoja na ufadhili wa miradi mingine miwili inayoongozwa na mashirika ya Canada.
Mkurugenzi wa Mradi huo Raphael Maligo ameeleza faida za mpango huo.
“Mbinu jumuishi ya huduma za afya ya uzazi na lishe inay tumiwa na mradi wa BRIGHT ni ya kipekee, badala ya kutoa huduma za afya ya uzazi na lishe katika vitengo tofauti,mradi huu unalenga kuhamasisha muunganiko wa huduma hizi muhimu kwa ustawi wa vijana. kwa kutambua kwamba huduma zote mbili zina uhusiano usioweza kutenganishwa na kuzitekeleza kwa pamoja husababisha faida kubwa na matokeo mazuri kwa afya ya vijana,” amesema Raphael Maligo.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa wakati wa tukio hilo, wasichana balehe mkoani Tabora wanakabiliwa na changamoto kubwa kiafya na ustawi wao.