Tanzania mguu sawa ukaguzi Afcon 2027

WAZIRI wa Utamaduni Sanaa na Michezo Dk Pindi Chana amesema Tanzania ipo tayari kwa ukaguzi unatakaofanywa na shirikisho la soka barani Afrika CAF ili kujiridhisha ikiwa Tanzania, Kenya na Uganda zipo tayari kuandaa Michuano ya Afcon 2027.
 
Hayo yamesemwa Julai 27,2023 Dar es Salaam katika hafla ya kutia saini mkataba wa ukarabati uwanja wa Benjamini Mkapa na Kampuni ya Beijing Construction Engineering Group (BCEG) itakayofanya ukarabati huo .
 
Dk Pindi Chana amesema lengo la ukarabati wa dimba la mkapa ni kuonesha utayari wa Tanzania kuandaa michuano hiyo mikubwa Afrika na dhumuni la serikali ni kuwa na uwanja wa kisasa utakaozivutia nchi nyingine.
 
“Serikali iliridhia ombi la kutaka kuandaa michuano ya Afcon ni lazima tuoneshe kwa vitendo utayari wetu na ndio maana leo tunaweka wazi makubaliano haya na Kampuni hii tunataka kuonesha kuwa tupo tayari, ukarabati ukikamilika tunatamani wengine wajifunze kupitia sisi” amesema Dk Chana.
 
Akielezea zaidi utayari wa Tanzania kulekelea ukaguzi huo utakaofanyika sambamba na ukarabati wa uwanja wa Benjamini mkapa Makamu wa pili wa Rais wa shirikisho la soka TFF Steven Mguto amesema shirikisho hilo litashughulikia ukarabati wa mabenchi ya Ufundi ya uwanja huo.
 
Aidha ameongeza kuwa shirikisho la soka barani Afrika CAF litagharamia matengenezo ya eneo la Kucheza ikiwa ni maandalizi ya michuano ya African Super League inayotarajiwa kutimua vumbi kuanzia mwezi oktoba mwaka huu ambapo klabu ya Simba itashiriki.
 
Wageni kutoka CAF wanatarajiwa kuingia nchini Julai 29 na kufanya ukaguzi kuanzia Julai 30 hadi Agost 1, katika viwanja vya Uhuru, na Benjamini Mkapa, uwanja wa ndege, na hospitali ya Taifa ya Muhimbili na kisha kufanya ukaguzi kama huo Zanzibar kabla ya kikao cha majumuisho kitakachofanyika Zanzibar ambacho kitashirikisha wawakilishi kutoka Tanzania Kenya na Uganda.
6 comments

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *