KIGALI; Rwanda, TIMU ya Taifa ya kuogelea ya Tanzania imeshika nafasi ya pili katika mashindano ya 8 Kanda ya Tatu ya kuogolea yaliyofanyika Kigali, Rwanda katika viwanja vya michezo Gahanga na kushirikisha nchi 10.
Tanzania sio tu wamefanya vizuri katika ushindi wa jumla, lakini hata waogeleaji kikosini wamenyakuwa tuzo mbalimbali binafsi ikiwemo makombe kwenye nafasi mbalimbali, hivyo kunyakua jumla ya medali 127 na makombe 8.
Waliotwaa medali za dhahabu katika makundi mbalimbali ya umri ni Collins Saliboko, Aryan Bhattbhatt, Max Missokia, Romeo Mwaipasi, Austin Okore, Filbertha Demello, Crissa Dillip, Muskan Gaikwad.
Waliotwaa medali za shaba na fedha ni Julius Missokia, Juanita viljoen, Amylia Chali, Natalia Ladha, Michael Joseph, Nicolene Viljoen, Bridget Heep, Delbert Ipilinga, Zainab Mosajee.
Kwa mujibu wa taarifa ya Ofisa Habari wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Najaha Bakari timu hiyo inatarajiwa kurejea nchini mchana huu, ambapo nchi zilizoshiriki na nafasi zao katika mabano ni Uganda (1), Tanzania (2) Kenya (3) Rwanda(4), Burundi (5), Afrika Kusini(6) Eswatini (7) Eritrea (8) Djibouti (9) na Ethiopia (10).