Tanzania yang’ara ubunifu kiuchumi Afrika

Tanzania

MIUNDOMBINU, matumizi ya teknolojia kukuza uchumi, soko la uhakika na uwepo wa nguvu kazi ya kutosha ni baadhi ya mambo yaliyoifanya Tanzania kushika nafasi ya 10 kati ya mataifa 54 barani Afrika kwa ubunifu wa kiuchumi.

Ripoti ya Viwango vya Maendeleo ya Ubunifu Duniani ya Mwaka 2022, toleo la 15 iliyotolewa na Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Wanataaluma Duniani (WIPO), Daren Tang mjini Geneva nchini Uswisi ilionesha kuwa mbali na Tanzania kushika nafasi ya 10 Afrika, taifa hilo la pili kwa ukubwa Afrika Mashariki limeshika nafasi ya 103 kati ya mataifa 132 yaliyoingizwa katika viwango hivyo vya kimataifa.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, vigezo vilivyotumika kubaini nafasi ya nchi ni pamoja na uwezo wa nchi kubuni na kutengeneza fursa za kiuchumi kwa wananchi wake, mazingira na ukuaji wa biashara ndani na nje ya nchi pamoja na utengenezaji wa mawazo ya kujenga uchumi kupitia teknolojia.

Advertisement

Ripoti hiyo imesema katika kipengele cha matumizi ya mtaji wa nguvu kazi, Tanzania imeshika nafasi ya 126 duniani huku upande wa miundombinu ikifanya vizuri zaidi kwa kushika nafasi ya 104 duniani wakati kwa upande wa matumizi ya taasisi kukuza uchumi ikishika nafasi ya 74 duniani.

Kwa upande wa soko la ukakika, Tanzania imeshika nafasi ya 79 duniani wakati ukuaji wa biashara ukiifanya nchi kushika nafasi ya 112 huku matumizi ya teknolojia yakiifanya nchi kuwa ya 114 duniani na kwa upande wa ubunifu taifa limeshika nafasi ya 94.

Kutokana na vigezo hivyo, ripoti hiyo ilionesha kuwa Tanzania inashika nafasi ya saba Afrika katika ukuaji wa pato ghafi la taifa na kwamba uchumi umefikia thamani ya dola za Marekani bilioni 207.

Mataifa yaliyoongoza Afrika kwa kuwa na ubunifu mkubwa wa kiuchumi ni pamoja na Mauritius (45) Afrika Kusini (61), Morocco (67), Tunisia (73), Botswana (86), Kenya (88), Misri (89), Ghana (95), Namibia (96) na Senegal (99).

Ripoti hiyo imeonesha mataifa yaliyoongoza kwa ubunifu wa kiuchumi duniani kuwa ni Uswisi, Marekani, Sweden, Uingereza, Uholanzi, Korea Kusini, Singapore, Ujerumani, Finland, Denmark, China, Ufaransa na Japan.

Mataifa kumi ya mwisho kati ya mataifa 132 yaliyojumlishwa ni pamoja na Msumbiji (123), Benin (124), Niger (125), Mali (126), Angola (127), Yemen (128) Mauritania (129), Burundi (130), Iraq (131) na Guinea (132).

1 comments

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *