TCAA: Mafunzo chuo cha TAC hayatambuliki

MKURUGENZI wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Hamza Johari amesema hawatambui mafunzo yanayotolewa na Chuo cha Tanzania Aviation College (TAC) chenye matawi katika mikoa ya Mwanza, Dar es Salaam na Arusha.
Johari alibainisha hayo jana kupitia taarifa aliyoitoa kwa umma na kusema kuwa usajili namba CAA/ ATO/050 ambao ulikuwa unatumiwa na chuo hicho uliisha muda wake tangu mwaka 2018.
Alisema chuo hicho kuendelea kutoa mafunzo ni kinyume cha taratibu za usajili iliyoainishwa kwenye Sheria ya Usafiri wa Anga, Sura ya 80 na kanuni zake.
Aidha, Johari alisema baada ya TCAA kujiridhisha kutokidhi viwango kwa chuo hicho pamoja na kutotambulika, amewataka wazazi wanaotaka kusomesha watoto masuala ya usafiri wa anga kujiridhisha kupitia tovuti yao, ili kutambua vyuo vinavyotambulika katika sekta hiyo.
“Mafunzo ya usafiri wa anga yanayoendeshwa na chuo hiki kwa mgongo wa kutambulika na TCAA ni kinyume cha sheria lakini pia wahitimu wa chuo wanakosa sifa ya kupata leseni kutoka TCAA hivyo kushindwa kupata ajira,” alisema Johari.