TCD wazindua Jukwaa la Wanawake

DAR ES SALAAM; Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD), leo kimezindua rasmi Jukwaa la Wanawake na wadau wa demokrasia nchini kwa lengo la kuongeza nguvu ya ushiriki wao kwenye siasa pamoja na kuwajengea uwezo wa kiuongozi.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa jukwa hilo, Mwenyekiti wa TCD Prof. Ibrahim Lipumba amesema litatumika kuleta usawa katika siasa na uongiozi.
Prof. Lipumba amewaomba wanawake wanasiasa wa vyama mbalimbali kulitumia kupaza sauti zao kwa pamoja juu ya masuala ya sheria, changamoto ambazo zimekuwa kikwazo kwao kushiriki chaguzi mbalimbali pamoja na masuala ya jinsia.
Uzinduzi huo ulihudhuriwa pia na Balozi wa Marekani nchini, Michael Battle na Balozi wa Uswisi nchini Didier Chassot, ambao walisema wameona nia safi ya Rais Samia Suluhu Hassan kudumisha demokrasia nchini.
Naye Katibu Mtendaji wa Jumuiya ya Wanawake Taifa wa Chama cha Wananchi (CUF), ambaye pia ni mwakilishi wa Jukwaa la Wanawake ,Anna Ryioba amesema jukwa hilo limezinduliwa wakati muafaka na kuwa watalitumia kueleza kasoro zilizopo kwenye chaguzi, ili siku zijazo mwanamke asidharauliwe na ashiriki kikamilifu.
Kituo cha Demokrasia Tanzania mbali na kuzindua leo Jukwaa la Wanawake, pia tayari kimeshaanzisha Jukwaa la Vijana lengo kutoa ushiriki sawa wa kidemokrasi katika kuhakikisha misingi imara inajengwa na kuimarisha demokrasia.