TIC wapewa maelekezo changamoto za wawekezaji

WAZIRI wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara Dk. Ashatu Kijaji amekitaka Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) kuhakikisha  wanatatua changamoto za wawekezaji katika maeneo yao, badala ya kuwasubiria wawekezaji ofisini kwa malalamiko.

Maelekezo hayo ameyatoa leo Juni 23, 2023 jijini Dar es Salaam katika hafla ya utiaji saini wa mikataba 10 ya utekelezaji wa miradi ya kimkakati na mahiri yenye thamani ya Dola za Marekani bilioni 1.805, ambayo sawa na Sh trilioni 4.32

“Serikali tumeshafanya kazi yetu, tunachohitaji kuona ni utekelezaji wa haraka wa majukumu ya mikataba hii kwa kuwa utiaji saini ni jambo moja na utekelezaji ni jambo lingine,” amesema.

Advertisement

Aidha, Dk. Kijaji amesema utiaji saini  wa mikataba hiyo ni matunda ya juhudi za Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, ambaye amekua  akitoa msukumo katika sekta binafsi na alihakikisha sheria ya uwekezaji ya 1997 iliyokuwa na ukinzani na Sheria ya fedha imebadilishwa, hivyo kupata Sheria mpya ya uwekezaji ya 2022.

Kwa upande  wa  Mkurugenzi Mtendaji wa TIC, Gilead Teri amesema kwa mara ya kwanza inashuhudiwa TIC ikitia saini mikataba 10 kwa pamoja ya utekelezaji wa miradi ya kimkakati na mahiri, ambayo itatoa ajira za moja kwa moja kwa watu  16,355 na zisizo za moja kwa moja watu 200,000.

“TIC tupo katika kuhakikisha tunatoa ushirikiano, kuboresha, na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma zetu ili miradi iweze kutekelezwa kwa wakati kama ilivyopangwa,” amesema

Naye, Meneja mradi wa Wild Flower and Oil Mills, Azizi Omary amesema, watahakikisha wanashirikiana na serikali katika kufikia lengo la kuzalisha mafuta ya kula nchini kwa asilimia 100 ifikapo 2027.

2 comments

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *