TIMU za Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela zimeanza vyema mashindano ya Umitashumta ngazi ya Mkoa wa Mwanza kwa kupata ushindi katika michezo mbali mbali ya mashindano hayo yanayoendelea katika viwanja vya Shule ya Nsumba mkoani hapa.
Katika mchezo wa mpira wa kikapu kwa wasichana Ilemela imeshinda kwa vikapu 20-8 dhidi ya Mwanza Jiji. Katika mpira wa pete,Ilemela imeshinda 40-13 dhidi ya Misungwi.
Kwa upande wa soka wavulana,Ilemela imeshinda kwa mabao 3-1 dhidi ya Magu na kwa wasichana Ilemela imeshinda kwa mabao 3-1 dhidi ya Buchosa.
Katika mchezo wa mpira wa wavu,Ilemela imeshinda seti 2-0 dhidi ya Magu. Katika mchezo wa mpira wa mikono Ilemela imetoka sare ya mabao 6-6 dhidi ya Kwimba na katika Soka Malumu ikatoka sare ya bao 1-1 dhidi ya Misungwi.
Naye Ofisa Michezo wa Manispaa ya Ilemela Kizito Bahati ameipongeza Manispaa yao kwa kupata ushindi kwenye michezo mbali mbali. Amesema wataendelea kupambana ili manispaa yao iweze kutwaa ubingwa wa jumla wa mashindano hayo.