“Taasisi ya Sekta Binafsi (TPSF) tumeanzisha dawati maalum la kushughulikia masuala ya mazingira Tanzania, ili kuhakikisha biashara zetu zinapata elimu inayofaa kutunza mazingira na kuendelea kupunguza kaboni.”
Kaimu Mkurugenzi wa TPSF, Raphael Maganga ameeleza hayo leo jijini Dar es Salaam wakati wa kongamano la wadau wa mazingira wanaohusika katika biashara ya kaboni ambayo ni uuzaji wa hewa ukaa.
Maganga amesema biashara hiyo ni mpya, hivyo lengo lake kubwa ni kwamba wakati wananchi wanalinda mazingira pia wanaweza kunufaika.
“Kama taasisi ya sekta binafsi tuna jukumu kubwa la kuhakikisha kuwa kila biashara Tanzania ina jukumu la kulinda mazingira, kupanda miti na kunufaika kutoka kwenye biashara hiyo au katika ulindaji wa mazingira.
“Viwanda vingi au kampuni nyingi duniani zinaharibu mazingira kwenye viwanda vinatoa moshi baadhi ya makubaliano yaliyofanyika mkataba wa Paris ni kwamba kampuni au taifa inaweza kupima ni kiasi gani cha hewa kinachafua mazingira.
“Kile kiasi inaweza ikaenda kwenye nchi nyingine ikawekeza kule ikapanda miti ili kuhakikisha kuwa kama tunatoa hewa chafu, ili tuzalishe hewa safi tuhakikishe mazingira yanatunzwa,” amesema.
Ameeleza kuwa mzalishaji wa hewa safi anapokea hela kwa kampuni au nchi ambazo zinatambulika tayari zinachafua mazingira, kwa hiyo fursa zipo nyingi kwa wananchi waendelee kupanda miti na kutunza mazingira.