TRC yaridhishwa ujenzi SGR Isaka, Mwanza
BODI ya Wakurugenzi wa Shirika la Reli Tanzania (TRC) limefanya ziara ya kukagua mradi reli ya mwendo kasi ya (SGR) kipande cha tano kutoka Isaka – Mwanza na kuridhishaa namna ya kasi ya ujenzi unavyoendelea.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo leo, Meneja mradi msaidizi kituo cha Mwanza -Isaka Moga Kulwa amesema kuwa mradi huo wa ujenzi umefikia 39%.
Amesema katika kipande cha tano cha Mwanza_Isaka kutakuwa na jengo abiria ambalo litakuwa na ukubwa wa sikwea mita 13000 na uwezo wa kuhudumia kuhudumia abiria 961 kwa wakati mmoja.
Kulwa amesema kuwa katika ujenzi huo wa reli ya kisasa kutakuwa na jengo la stesheni ambalo linajengwa pembeni yake kuhakikisha miundombinu ya reli ya zamani inaboreshwa na kutakuwa na daraja la juu linajumla ya kilomita 1.4 na mkandarasi anaendelea na kazi na mpaka sasa limefikia 35.51%.
“Mpaka hivi sasa mradi wetu tunategemea ukamilike mwaka 2024 mwezi wa Mei na mradi huu utawasaidia sana wafanyabiashara kwasababu usafiri huu utakuwa unatumia masaa 8 toka Mwanza -Dar es salaam na usafiri wetu utakuwa wa bei ya chini’’ amesema Kulwa.
Mwenyekiti wa bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la reli nchini(TRC) Ally Karavana amesema mradi unaendelea vizuri Watanzania watarajie mradi utakamilika kwa wakati. Karavana amesema faida kubwa za mradi huo ni utabadirisha uchumi wa nchi kwenda kwenye uchumi wa kati.
Naye Kaimu Mkurugenzi wa Shirika la Reli (TRC) Amina Lumuli amesema lengo la ziara hiyo ni kuipa uelewa bodi mpya ya wakurugenzi kuhusu mradi wa Sgr na walianzia kipande cha kwanza cha mradi huo kilichopo Dar es salaam na kumaliza kipande cha tano Mwanza.
Lumuli amesema kuwa vipande vyote vinaendelea vizuri na hakuna kipande kilichosimama na utengenezaji wa mabehewa unaendelea vizuri hakuna shida yoyote. Amesema kichwa cha kwanza cha treni kinatarajia kuingia nchini mwezi Novemba mwaka huu.
“Utengenezaji wa mabehewa unaendelea vizuri nadhani mtakuwa mashahidi kwamba tumeshapokea mabehewa 14 mapya.’’ amesema Lumuli.