DODOMA: WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa, amesema serikali inaendelea na mpango mkakati wa ujenzi wa vituo vya ukaguzi katika maeneo mbalimbali kwa lengo la kuimarisha usalama wa nchi na ukusanyaji mapato.
Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo bungeni leo Mei 30,2024, alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Biharamulo Magharibi, Mhandisi Ezra Chiwelesa kwenye kipindi cha maswali ya papo kwa papo kwa Waziri Mkuu, aliyetaka kujua mpango wa Serikali kukamilisha ujenzi wa vituo vya ukaguzi katika maeneo ya Vigwaza, Dumila, Manyoni na Nyakanazi.
SOMA: Vituo vya kisasa vya ukaguzi wa magari kujengwa mipakani
Akijibu swali hilo, Waziri Mkuu amesema Serikali inaendelea na mpango mkakati wa ujenzi wa vituo vya ukaguzi katika maeneo ya Vigwaza, Dumila, Manyoni na Nyakanazi lengo likiwa ni kuimarisha usalama wa nchi, ukusanyaji wa mapato na kuondoa usumbufu kwa wasafirishaji kukaguliwa kila mahali kwa kuwa vinajengwa kwa umbali ambao hauwezi kuleta usumbufu.
Pia amesema Serikali inaendelea na mpango wa kuziimarisha bandari za Mtwara, Tanga na ujenzi wa bandari ya Bagamoyo pamoja na kuhamasisha mataifa ya nje kutumia Bandari ya Dar es Salaam.
“Hii itasaidia nchi nyingi kutumia bandari zetu ambayo itasadia kuimarisha ukusanyaji wa mapato,” amesema Waziri Mkuu.