ARUSHA; RAIS wa Zanzibar, Dk. Hussein Ali Mwinyi amesema serikali itaendelea kuweka mazingira mazuri ya biashara katika sekta binafsi, ili kusaidia kukuza uwekezaji.
Akifungua mkutano wa 29 wa wanahisa wa Benki ya CRDB, Rais Mwinyi amesema serikali inajivunia uwepo wa taasisi kubwa za fedha kwa ajili ya umarishaji uchumi hususani uchumi wa buluu
Amesema kupitia programu za uwezeshaji ya ‘Inuka na Uchumi Wetu’ kwa upande wa Zanzibar, benki hiyo imechangia katika uendelezaji sekta mbalimbali zikiwemo utalii, kilimo, ufugaji, uvuvi, biashara na ujasiriamali.
Amesema ushirikiano mzuri kati ya CRDB na taasisi mbalimbali za serikali umechangia uunganishwaji wa mifumo ya kodi na tozo za serikali, jambo lililoongeza ufanisi katika ukusanyaji mapato
“Benki ya CRDB mnaendelea kujidhihirisha kwa vitendo kuwa mnaenzi Muungano na pia tunawashukuru kwa kujali wanahisa pamoja na kushirikiana na serikali,” amesema.
Amesema uwepo wa mazingira rafiki ya biashara utasaidia serikali kukuza uwekezaji katika biashara na ongezeko la uwekezaji katika hisa kupata thamani.
“Serikali inafurahia mafanikio ya benki hii na naipongeza menejimenti ya benki ya CRBD kwa kutoa semina kwa wanahisa kwa ajili ya kujua umuhimu wa uwekaji hisa, kwani fedha ni nyenzo muhimu ya maendeleo ya Taifa,” amesema.
Kwa upande wake Waziri wa Fedha Zanzibar, Saada Mkuya Salum, amesema benki ya CRDB imekuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha uchumi wa Zanzibar unakua kutokana na benki hiyo kuchagiza maendeleo, ikiwemo ujenzi wa miundombinu mbalimbali.