UNFPA kusaidia uchakataji, ukamilishaji takwimu za sensa

SHIRIKA la Umoja wa Mataifa la Idadi ya Watu (UNFPA) limeahidi kuendelea kuisaidia Tanzania kupitia Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) kuendelea kufanya uchakataji na ukamilishaji wa takwimu za Sensa ya Watu na Makazi iliyofanyika Agosti 23, mwaka huu.
Matokeo ya mwanzo ya Sensa ya Watu na Makazi yalitangazwa rasmi na Rais Samia Suluhu Hassan, Oktoba 31, mwaka huu.
Akizungumza wakati wa kuaga maofisa wa NBS jijini hapa, Naibu Mwakilishi Mkazi wa UNFPA nchini, Wilfredy Ochan alipongeza kazi nzuri iliyofanywa na NBS, lakini akaahidi kwenda kusaidia suala la uchakataji wa takwimu.
“UNFPA itaendelea kusaidia uchakataji na ukamilishaji wa takwimu hizo unaofanywa na NBS kwa lengo la kuhakikisha zinakamilika na kutumika na taasisi mbalimbali nchini wakiwemo watu binafsi, mashirika na serikali katika kutekeleza Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025 na Mipingo ya Maendeleo nchini,” alisema.
Achan akinukuu kauli ya Kamishna wa Sensa, Anne Makinda alisema kwamba UNFPA imechangia Euro 200,000 kwa ajili ya kusaidia NBS kuhakikisha takwimu zinachakatwa ili kutumiwa katika mipango mbalimbali ya maendeleo ya nchi.
Ochan ambaye alichaguliwa kuwa mwakilishi mkazi wa Shirika la Idadi ya Watu nchini Ghana, alisisitiza kwamba shirika hilo limetilia mkazo kwamba NBS inahitaji msaada wa kisasa wa kuchakata takwimu na kuzitumia katika kuhabarisha umma kuhusu mpango wa maendeleo wa 2025 na kufanya marejeo ya kitaifa ya mpango wa maendeleo.
“Tunaiahidi NBS kuendelea kufanya kazi pamoja kwa sababu tuna ushirikiano wa kudumu, tutashawishi washirika wengine kusaidia uchakataji wa takwimu zaidi, lakini pia tutaangalia njia ya kusaidia sisi wenyewe,” alisema.
Alisema kwa yeye kuwapo Ghana kunaleta matokeo mazuri ya kutengeneza mtandao wa mawasiliano na Tanzania na hivyo fursa nyingi zinapatikana kupitia mtandao.
“Ghana imefanya sensa ya kidijitali mwezi Mei mwaka huu lakini pia inaweza kuwa fursa ya Tanzania kujifunza kutoka kwetu, kama watakuwa wanataka kufanya nitakuwa mratibu wa kuhakikisha wanafanikiwa,” alisema.
Aliwashukuru wafanyakazi wa NBS kwamba amejifunza kutoka kwao kuwa na uongozi imara na timu imara na kutokana na uwezo wa NBS ndio maana wameweza kutoa sifa nzuri kwa taifa ambazo si za kawaida.