DIRISHA la upigaji kura katika tuzo za Chaguo la Mteja Afrika mwaka 2023, litafunguliwa rasmi Jumatatu Oktoba 9, na kufungwa Novemba 2, mwaka huu.
Imeelezwa kuwa tangu kuanza kwa tuzo hizo mwaka 2019, zimechochea kampuni mbalimbali nchini kuongeza ubunifu, ushindani na kuzalisha huduma na bidhaa bora kulingana na mahitaji ya soko.
Akitoa taarifa kwa waandishi wa habari, Dar es Salaam, mwanzilishi wa tuzo hizo, Diana Laizer amesema baada ya upigaji kura tuzo hizo zitatolewa Novemba 11, mwaka huu katika ukumbi wa The Superdome Masaki, Dar es Salaam.
Amesema kuwa mifumo ya upigaji kura katika tuzo hizo, inasimamiwa na wataalamu wa ukaguzi wa ndani ambao ni Auditax International hivyo, aliwataka wateja kuhakikisha wanapiga kura kupata kampuni wanazohitaji.
Laizer amesema katika kipindi hiki, kampuni zimekuwa zikijinadi na kuelezea ubora wao na kuongeza ushindani kwa kampuni ili wateja wao waweze kuwachagua.
“Tuzo hizi zilianza kutolewa mwaka 2019 zikijulikana kama tuzo za Chaguo la Mteja Tanzania (Consumer Awards Tanzania) na baadae mwaka 2021 zilibadilika na kuhusisha bara zima la Afrika,” amesema.
Ameeleza kuwa huu ni mwaka wa tano tangu kuanzishwa kwa tuzo hizo na kwamba kwa kushirikiana na Wizara ya Viwanda na Biashara chini ya Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade) wamefanikiwa kuchochea kampuni nyingi kubuni huduma na bidhaa bora.
Amesema tuzo hizo zinamthamini mteja zikimfanya kama mwamuzi mkuu katika soko kwa kuipa kampuni nguvu ya kuendelea kutoa huduma na kufikiria vitu vipya.
“Tunaamini kuwepo kwa hizo tuzo kumeongeza chachu kwa kampuni kuongeza ubunifu, ushindani na ubora katika utoaji wa huduma na bidhaa na kwa kupitia TanTrade wametusaidia kuhakikisha , ” amesisitiza Laizer.
Ameongeza kuwa mchakato rasmi wa tuzo hizo ulianza Juni ambapo walizindua na kupokea mapendekezo ya kampuni kupitia mtandao.
Ameeleza kuwa timu majaji kutoka TanTrade waliahakikisha majina yaliyopendekezwa yanaendana na soko lililopo.
Amefafanua kuwa kipindi cha upigaji kura kinampa fursa mteja kupigia kura kampuni anayoona imemridhisha katika utoaji wa huduma zake.
Mkaguzi wa Mifumo wa Auditax International, Alex Nzanda amesisitiza kuwa wanahakikisha uaminifu na uhakika wa kura zitakazopigwa na wateja na kisha kuzichakata ili kupata washindi.
Ameeleza kuwa ni wajibu wa wateja kushiriki katika upigaji kura ambao utafanyika kwa njia ya mtandao.
“Kabla ya kupiga kura mfumo utahitaji barua pepe yako na kisha kukutumia kiunganishi (Link) kitakachokupeleka moja kwa moja kwenye ukurasa wa watoa huduma wanaoshindana na utachagua kisha kura itahesabiwa kwenye mfumo huu,”
Nzanda amesema wateja wanachotakiwa ni kujitokeza kwa wingi kupiga kura Ili kuchagua kampuni wananzozipenda na zilizofanya vizuri katika biashara.
Kwa upande wake, Fredrick Bundala kutoka Simulizi na Sauti, amesema kampuni zinaweza kujitangaza kupitia chombo hicho na kuelezea huduma na bidhaa zao na kwa nini wapigiwe kura.
Amesema kampuni hizo zinaweza kujitangaza kupitia mitandao yao ya kijamii ikiwemo YouTube, Instagram, Twitter na website ili wawafikie wateja wao kwa urahisi na kwa gharama nafuu.
Comments are closed.