Upimaji; tiba inayorejesha faraja kwa wenye Ukimwi

MBAYE (si jina halisi) alijivunia mafanikio makubwa ya kimaisha aliyopata mwaka 2019. Lakini mwaka 2020, alijikuta katika simanzi kutokana na mabadiliko ya afya. Nguo zilianza kumpwaya.
Alipokwenda kupima afya, alibaini kuwa na maambukizi ya virusi vya Ukimwi. Mkewe, aliyekuwa mjamzito, pia alipima na kujikuta na maambukizi.
Wanandoa hao walisafiri kutoka eneo walilokuwa wakiishi kwenda mji wa Dakar ambao ni makao makuu ya nchi ya Senegal kupata dawa za kufubaza virusi (ARVs). Walipata pia huduma ya kuzuia maambukizi ya mama kwenda kwa mtoto aliye tumboni.
Ilikuwa furaha kubwa kwa Mbaye na mkewe kwani licha ya afya yao kurejea katika hali ya kawaida, vilevile mtoto aliyezaliwa, alipopimwa hakuwa na virusi vya Ukimwi.
Simulizi hii ilitolewa na Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika, Dk Matshidiso Moeti, kupitia ujumbe wake wa maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani. Dunia huungana kuadhimisha siku hii kwa kuangalia maendeleo ya mapambano ya Ukimwi.
Huainisha changamoto na kuweka mikakati ya kukomesha janga hili. Akirejelea kisa hicho cha wanandoa, Dk Moeti anasema kinakumbusha umuhimu wa serikali na wadau wa masuala ya afya kutoruhusu Ukimwi kushuka kwenye orodha ya vipaumbele Afrika.
WHO kupitia kwa Moeti inahimiza kuendeleza huduma za kuzuia VVU, upimaji na tiba kwa kuzingatia usawa wa makundi yote ya watu bila kuacha yeyote nyuma.
“Tunaunga mkono watu waishio na HIV na kuwakumbuka waliopoteza maisha kutokana na Ukimwi. Kaulimbiu ya mwaka huu ni ‘Usawa’ ikitaka kila mmoja kuhimiza usawa katika juhudi za kukabili ugonjwa,” anasema.
Anaeleza kuwa Kanda ya Afrika, ina watu wapatao milioni 25.6 wanaoishi na VVU na kwamba katika muongo uliopita, maambukizi mapya yamepungua kwa asilimia 44 na vifo vitokanavyo na maradhi hayo vimepungua kwa asilimia 55. Anasema mafanikio yamekuwapo kwa sababu ya hatua mbalimbali ambazo WHO na wadau wamekuwa wakifanya ikiwamo kuhimiza na kuunga mkono upanuzi wa teknolojia mpya za kuzuia na tiba kwa ugonjwa huu.
Hatua nyingine ni kutoa mwongozo wa kuunganisha kinga, upimaji na tiba; kuzijengea uwezo nchi kuboresha upatikanaji wa takwimu na ubora.
Shirika hilo na wadau pia wameongeza wigo wa kupata dawa, tiba teknolojia za kiafya. Pia wanaunga mkono mipango ya kitaifa ya tiba ya HIV na WHO inazitaka nchi na wadau kuziba pengo la usawa kutokomeza Ukimwi kwa kujielekeza kwenye makundi yaliyoachwa nyuma.
“Tunapaswa kuhakikisha kwamba, kila mmoja anakuwa na usawa katika kupata kinga, vipimo, tiba na huduma za HIV,” anasema Dk Moeti.
Anasisitiza wizara zenye dhamana ya afya katika nchi wanachama kujenga mifumo imara ya afya inayotekelezeka itakayoweza kubaini mambo yasiyo na usawa na kutoa suluhisho.
Ikiwa imebaki miaka minane kufikia mwaka 2030 ambao umelengwa Ukimwi uwe umetokomezwa, Moeti anasema panahitajika hatua za kukomesha athari zitokanazo na janga hili kwa kujielekeza kwa makundi yaliyoathirika hususani watoto, vijana balehe wa kike, wanawake na makundi mengine.
Nchi wanachama wa shirika hilo zikiungwa mkono na wadau, zinatakiwa kupanua na kuendeleza upatikanaji wa huduma za kinga na tiba kwa watu wote kwa kutumia mifumo ya utoaji wa huduma za kiubunifu. Kinga, tiba Tanzania Nchini utoaji kinga na tiba unafanyika kutokana na huduma za kibunifu ikiwamo utoaji wa dawa tiba ya sindano kwa watu wenye VVU, utoaji dawa rafiki za ARVs kwa watoto na uwezeshaji watu kujipima VVU.
Sindano kinga Katika mahojiano maalumu na HabariLEO kwenye maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani yaliyohitimishwa mjini Lindi, Ofisa wa WHO Tanzania-Ukimwi, Kifua Kikuu na Homa ya Ini, Dk Johnson Lyimo anataja sindano kuwa ni miongoni mwa dawa kinga za muda mrefu, zenye mafanikio makubwa.
Dk Lyimo anasema Oktoba mwaka huu, WHO ilipendekeza kuanza kutumika kama dawa kinga inayozuia maambukizi ya Ukimwi (PReP).
“Mapendekezo ya WHO yalishatoka kwamba zianze kutumika kwa nchi yetu. Sasa hivi tunaendelea kushauriana na serikali na mashirika yanayodhamini mpango …ili kuanza kuzitumia nchini. Na katika matumizi yake, wanaweza kuanza kwenye maeneo baadhi, halafu ikaongezeka kwa ukubwa,” anasema.
Anafafanua zinavyotumika: “Kikubwa sana kwenye upande wa sindano, ukiichoma leo, unachoma tena baada ya miezi miwili. Na tafiti za awali zimeonesha kwamba imekuwa na kinga kubwa sana. Wagonjwa wanaochoma sindano wanapata kinga kubwa sana ya HIV.”
Hata hivyo, anasema zipo changamoto hususani usugu wa dawa, hivyo inashauriwa dawa hizo zitumike huku mfumo wa ufuatiliaji usugu wa dawa ukiimarishwa katika vituo na sehemu mbalimbali. Kwa mujibu wa mtaalamu huyo, WHO imeshatoa mwongozo wa kufuatilia usugu wa dawa. Anasema watakaa na wahisani, wadau kwa ajili ya kutekeleza mpango huo wa kufuatilia usugu wa dawa wakati zikiendelea kutolewa. Wanaostahili kutumia sindano ni watu wazima pekee na si kwa watoto.
“Kumbuka kwamba hizi ni sindano kinga, kwa hiyo ina maana ni kwa wale walio katika hatari ama kitabia au kimazingira. Mfano baba au mama, mmoja ana virusi na mwingine hana…Ikifika katika umri balehe na umri wa juu wa kushiriki ngono tunawaongeza.” Lengo ni kuweka nguvu katika kupunguza maambukizi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto kutoka asilimia 11 za sasa hadi asilimia tano.
ARVS ZA WATOTO
Kuhusu ARVs rafiki kwa watoto wadogo, Dk Lyimo anasema zimeanza kusambazwa nchini. Anasema kuanza kwake ni hatua kubwa katika muktadha mzima wa tiba ya Ukimwi kwa watoto.
Anasema ipo dawa mpya iitwayo DTG 10 na kuanzia Mei mwaka huu, watumishi katika mikoa yote wamepata mafunzo juu ya namna ya kuitumia.
“Tayari zimeanza kusambazwa katika mikoa yote. Dawa hii imeshasambaa mikoa yote nchini, matumizi yake yameanza. Hili ni eneo mojawapo tulilopiga hatua. Lakini linahitajika ufuatiliaji.”
KUJIPIMA HIV
Kuhusu vipimo vya kujipima virusi, Dk Lyimo anasema huo ni mkakati muhimu unaotarajiwa kuwezesha kufikia makundi kirahisi.
Hata hivyo, anasisitiza kuwa majibu yanayopatikana si ya mwisho, bali mhusika anapaswa kwenda kwenye vituo kuyahakiki. Mtaalamu huyo anasisitiza mambo ya kuwekea msisitizo ni pamoja na eneo la kinga kwa maana ya mama kwenda kwa mtoto kama ambavyo Mbaye na mkewe walifanikiwa kumlinda mtoto wao na kurejesha furaha ndani ya familia.