MAREKANI: Makumi ya nchi za Magharibi zimeungana na Ukraine, Uingereza na Marekani kulaani madai ya kuwepo kwa makubaliano ya uhamishaji wa makombora ya balistiki kati ya Korea Kaskazini na Urusi, ambayo walisema ni ukiukaji wa vikwazo vya Umoja wa Mataifa kwa Korea Kaskazini.
Katika taarifa ya pamoja, mkuu wa sera za kigeni wa Umoja wa Ulaya Josep Borrell, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Antony Blinken na mawaziri wa mambo ya nje kutoka nchi 47 zikiwemo Argentina, Australia, Guatemala, Japan na Korea Kusini, wamelaani madai hayo kwa kwa nguvu zote, wakisema silaha hizo tayari zimetumika dhidi ya Ukraine mnamo Desemba 30 na Januari 2.
“Uhamisho wa silaha hizi unaongeza mateso ya watu wa Ukraine, unaunga mkono vita vya uchokozi vya Urusi na kudhoofisha mpango wa kimataifa wa kutoeneza silaha,” ilisema taarifa hiyo iloyotolewa leo, ikibainisha kuwa ushirikiano huo pia utatoa mafunzo ya kijeshi kwa Korea Kaskazini.
Taarifa hiyo pia ilisema nchi hizo zina wasiwasi na tishio la kiusalama ambalo ushirikiano huo unaweza kuleta katika Mataifa ya Ulaya, Rasi ya Korea, katika eneo la Indo-Pacific, na duniani kote,
Awali, msemaji wa Baraza la Usalama la Kitaifa la Marekani, John Kirby alisema Urusi imetumia silaha nyingi za Korea Kaskazini nchini Ukraine, ikiwa ni pamoja na zile zilizotumika kushambulia Kharkiv, mji wa pili kwa ukubwa nchini Ukraine.
Marekani na washirika wake wanapanga kulipeleka suala hilo katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa (UNSC) baadae leo hi, aliongeza Kirby
Taarifa hiyo iliongeza kuwa ununuzi na usambazaji wa silaha kati ya Pyongyang na Moscow ulikiuka maazimio ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa yaliyowekwa mwaka 2006 kufuatia mpango wa silaha za nyuklia wa Korea Kaskazini.
Hata hivyo Msemaji wa Ikulu ya Urusi Kremlin, Dmitry Peskov alikataa kutoa maoni yake alipoulizwa kuhusu madai hayo