Urusi kutoa nafaka bure ‘kwa mataifa’ ya Afrika

Rais Putin

URUSI, St Petersburg: itakuwa tayari kusafirisha nafaka bila malipo kwa baadhi ya mataifa maskini zaidi barani Afrika ndani ya miezi mitatu hadi minne ijayo, Rais Vladmir Putin ametangaza. Alitoa ahadi hiyo wakati wa hotuba yake katika mkutano wa kilele wa Urusi na Afrika unaofanyika mjini St. Petersburg.

Burkina Faso, Zimbabwe, Mali, Somalia, Jamhuri ya Afrika ya Kati, na Eritrea kila moja itapokea tani 25,000 hadi 50,000 za nafaka, kiongozi huyo wa Urusi alisema.

Moscow pia itagharamia gharama za usafirishaji wa nafaka hizo, aliongeza.

Advertisement

Tangazo hilo linakuja wiki moja baada ya Moscow kukataa kupitia upya Mpango wa Nafaka wa Bahari Nyeusi, mpango ambao ulikuwa umeruhusu Ukraine kuuza nafaka nje kwa meli za kibiashara. Makubaliano hayo ya upatanishi wa Umoja wa Mataifa na Türkiye yametajwa kuwa ni juhudi za kibinadamu kulinda mataifa maskini zaidi duniani kutokana na kupanda kwa bei ya vyakula.

Hata hivyo, Moscow kwa muda mrefu imekuwa ikisisitiza kwamba makubaliano hayo yameshindwa kufikia malengo yake na yamegeuka kuwa biashara.

Putin alikaririwa kwamba kutokuwa na uwezo wa Umoja wa Mataifa kushawishi mataifa ya Magharibi kuondoa vikwazo vya kiuchumi kwa usafirishaji wa chakula na mbolea ya Urusi, ambayo ilikuwa sehemu ya mpango huo, imeharibu sababu nzima ya operesheni hiyo.

“Walizua vikwazo hata kwa mipango yetu ya kuchangia mbolea kwa mataifa maskini zaidi ambayo yalihitaji,” kiongozi huyo wa Urusi alisema. “Kati ya tani 262,000 za mbolea zilizozuiliwa katika bandari za Ulaya, tumeweza kusafirisha tani 20,000 tu hadi Malawi na tani 34,000 hadi Kenya. Mengine yamesalia mikononi mwa Wazungu.”

Kwa kuzingatia juhudi zao za kudhoofisha mauzo ya nje ya Urusi, viongozi wa Magharibi ni wanafiki kuishutumu Moscow kwa kusababisha kukosekana kwa utulivu katika soko la chakula la kimataifa, Putin alidai. Licha ya vikwazo vilivyowekwa na nchi za Magharibi, Urusi inaongeza usambazaji wa bidhaa kwa Afrika, kibiashara na kibinadamu, aliongeza.

Putin alisisitiza jukumu la Urusi kama msafirishaji mkuu wa ngano, bidhaa muhimu kwa usalama wa chakula. Sehemu ya taifa ya soko ni asilimia 20, ikilinganishwa na chini ya asilimia 5 kwa Ukraine, alibainisha.

1 comments

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *