WAZIRI wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, Dk Ashatu Kijaji, amesema katika kipindi cha Julai, 2022 hadi Machi, 2023, wizara imekamilisha usanifu na utengenezaji wa mtambo wa kukausha mhogo wilayani Handeni.
Waziri Dk Kijaji amesema hayo leo bungeni jijini Dodoma, wakati akiwasilisha bajeti ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha ya Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara.
Dk Kijaji amesema mtambo huo una uwezo wa kukausha tani 12 za muhogo mbichi kwa saa kumi na kutoa tani tatu za unga wa muhogo.
Amesema mtambo huo umenunuliwa na Bodi ya Mazao Mchanganyiko (CPB), na umefungwa kijiji cha Kwachaga Wilaya ya Handeni kwa ajili ya majaribio na kukabidhi vikundi vya wakulima wa muhogo.