MECHI ya Ligi ya Mabingwa kati ya Simba SC na Wydad AC itaamuliwa kwa usaidizi wa picha za video (VAR) ambapo maafisa wake watakuja kesho. Ameeleza Ofisa Habari na Mawasiliano wa Simba, Ahmed Ally.
Akizungumza na wanahabari leo Aprili 18, 2023 Ahmed Ally amesema mchezo huo utapigwa Jumamosi saa 10:00 jioni Uwanja wa Mkapa Dar es Salaam, hasa baada ya kupeleka maombi CAF kuhusu kubadilishiwa muda wa mchezo.
“Mnakumbuka mechi za makundi tulicheza saa 1 usiku lakini mechi hii tumepata saa 10 na hilo ni baada ya kuwaomba CAF sababu itakuwa sikukuu ili kila Mwanasimba aje uwanjani”. amesema Ahmed Ally.
Ahmed amesema kiungo Sadio Kanoute anasumbuliwa na nyonga na leo atawasili kambini kukutana na madaktari kama atakuwa sawa ataanza mazoezi, hivyo hivyo kwa Aishi Manula atakutana na madaktari kuangalia hali yake.