DODOMA: WIZARA ya Afya kwa Kushirikiana na Ofisi ya Rais TAMISEMI imesambaza vifaa zaidi ya milioni 1.6 vya mtu kujipima mwenyewe maambukizi ya virusi vya ukimwi.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Afya Ummy Mwalimu jijini Dodoma ambapo amesema Wizara ya Afya kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais TAMISEMI itaendelea kuongeza nguvu za kusambaza vifaa hivyo vya watu kujipima wenyewe virusi vya ukimwi ili kuweza kutambua hali zao wenyewe na kwa haraka kuhusu ugonjwa huo.
Amesema, Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan imeendelea kupanua wigo wa vituo vya kupima na kutoa huduma za matunzo (CTC) kwa watu wenye ukimwi ambapo hadi sasa kuna vituo 8,529.
Pia, amesema Serikali kupitia Wizara ya Afya pamoja na Ofisi ya Rais TAMISEMI itaendelea kutoa huduma za kupima, tiba na matunzo kwa watu wanaoishi na VVU hapa nchini ili vituo vyote vinavyotoa huduma za Afya viwe pia vituo vya kupima na kutoa matunzo (CTC) kwa asilimia 95 ifikapo mwaka 2025.
Aidha, amesema chini ya uongozi mahiri wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Serikali itaendelea kuhakikisha upatikanaji wa dawa na vitendanishi kwaajili ya watu wanaoishi na virusi vya ukimwi ikiwemo kuendelea kufuatilia taarifa zote kuhusu uwepo wa dawa mpya ambazo ni bora zaidi.