MKEMIA Mkuu wa Serikali, Dk Fidelice Mafumiko, amesema kuwa takwimu za Shirika la Afya Duniani, zinaonesha kuwa vifo vinavyotokana na madhara ya kemikali vimeongezeka.
Amesema takwimu hizo zinaosha kwa mwaka 2012 kulikuwa na vifo vya watu milioni 1.3, mwaka 2016 vifo milioni 1.6 na mwaka 2019 vilikuwa vifo milioni 2.
Akizungumza jijini Dar es Salaam wakati wa kufunga semina ya wadau wanaotumia kemikali, ikiwa na lengo la kuwaelekeza jinsi mfumo wa Dunia wa pamoja wa matumizi ya kemikali unavyofanya kazi.
Dk Mafumiko amewataka watumiaji wa kemikali kufuata sheria na kanuni, ili kuepuka madhara na vifo.
Pia amesema faida kubwa ya mafunzo hayo ni kuwawezesha wataalamu kutoka taasisi za serikali na binafsi kuwa na uelewa.
“Sasa wakielewa wote kuwa kemikali tunapoleta nchini, kusafirisha na kutoa zina mfumo wa utambuzi wa pamoja wa Dunia utajenga watu kutekeleza majukumu kwa kuzingatia sheria na kanuni hapa tunaangalia kemikali hususan zenye madhara kwa afya na mazingira, yaani kemikali hatarishi,”ameeleza.
Amesema mafunzo hayo yamewezeshwa na maabara ya mkemia mkuu wa serikali kwa kushirikiana na shirika la umoja wa mataifa linaloshughulikia utafiti, ambalo limeweza kuwapa wataalamu wawili kufundisha mada zinazohusiana na ujengaji wa uelewa wa pamoja kuhusu mfumo huo wa kidunia wa pamoja.