Vijana washauriwa kuwa wabunifu

MHITIMU wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Geshom Munyi amewashauri vijana kutofikiria vyeti wanapohitimu masomo yao bali wafikirie ni jinsi gani wataweza kuzalisha bidhaa zitakazotatua changamoto katika jamii.
Munyi ambaye amehitimu mwaka 2019 kozi ya ualimu, ni miongoni mwa wanufaika 49,000 wa Mfuko wa Kuendeleza Ujuzi kupitia Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA), alitoa ushauri huo katika Maadhimisho ya Juma la Elimu la Watu Wazima kitaifa yanayofanyikia Kibaha Pwani.
Amesema endapo vijana wakijituma fursa zipo nyingi kinachotakiwa ni kuchungulia zilipo na kuzifanyia kazi bila kukata tamaa.
Amesema alipomaliza masomo yake aliweza kuajiriwa baada ya muda mfupi aliacha kwa kuwa hakuona faida ya kile alichokuwa anakifanya, hivyo alipopata fursa hiyo kutoka TEA aliitumia katika eneo la utengenezaji wa viungo mbalimbali.
“Nimenufaika kupitia Sido ambapo huo mradi ulitoa fedha ili tujifunze, niliamua kujifunza usindikaji wa viungo japo nimesomea ualimu,” amesema.
Amesema alianza kwa kusindika tangawizi kilo 20 lakini hivi sasa anafikia kati ya kilo 700 na 800,” alisema na kuongeza kuwa hivi sasa anasindika pia mdalasini, viungo vya chai, iliki, karafuu, pilipili manga pamoja na biskut za tangawizi.
“Nimefanikiwa kujiajiri pia nimeweza kuajiri wahitimu wengine wa chuo kikuu,” amesema.
Ametaja soko lake kubwa lipo mikoa ya Iringa, Dodoma, Dar es Salaam, Mwanza, Mbeya na Zanzibar.
“Lakini sasa hivi ninachokiona ni pesa tu ambazo zipo mbele sasa hivi nikipata mtaji siwezi kupoteza nirahisi kuulinda ninajua mianya yote inayoweza kupoteza mtaji kwa namna ya kuweza kulinda mtaji,” amesema.
Kwa upande wake Ofisa Uhusino kutoka TEA, Eliafile Solla amesema mamlaka hiyo inashiriki kwenye maonesho hayo kupitia mfuko wake huo ambao unalenga kukuza na kuendeleza ujuzi katika sekta sita za kipaumbele.
Ametaja sekta hizo kuwa ni nishati, Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (Tehama), ujenzi, uchukuzi, kilimo, utalii na huduma za ukarimu.
“Kupitia mfuko huo mafunzo yanayotolewa yapo nje ya mfumo rasmi na juma la elimu ya watu wazima linalenga kuangalia mchango wa mafunzo yanayotolewa nje ya mfumo rasmi unavyosaidia kwenye jamii na ndio maana TEA wako hapo,” amesema.
Ameeleza wanufaika waliopata ujuzi kupitia mfuko huo wengi wameweza kujitengenezea kipato lakini pia wameweza kuwaajiri vijana wengine.
Amesema kwa miaka mitano ya mfuko huo, umewezesha kunufaisha watanzania 49,000.