UAMUZI wa Rais Samia Suluhu Hassan kutoa vishikwambi kwa walimu na wadhibiti ubora nchini umeleta mchango mkubwa katika kuleta mageuzi makubwa katika sekta ya elimu nchini.
Vishikwambi hivyo takribani 300,000 vilivyotumika katika Sensa ya Watu na Makazi Agosti 23, mwaka huu, 293,400 vinagawiwa kwa walimu kwa lengo la kuboresha ufundishaji wanafunzi katika shule mbalimbali nchini.
Akizungumza Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda alisema Rais Samia ametoa vishikwambi hivyo kwa walimu ili kuleta mageuzi makubwa ya elimu nchini.
Profesa Mkenda alisema Tehama ni chanzo cha maendeleo ya kijamii na kiuchumi na hasa katika kukuza kasi ya teknolojia nchini.
Vishikwambi hivyo vinalenga kuboresha elimu nchini kwa kuwapa unafuu katika ufundishaji na ujifunzaji wanafunzi shuleni.
Profesa Mkenda alisema walengwa ni walimu wa shule ya msingi na sekondari, wadhibiti ubora wa elimu, wakufunzi, walimu wa vyuo vya ufundi na vyuo vya maendeleo ya jamii.
Naye Victoria Kishua alisema vishikwambi hivyo ni msaada mkubwa katika kufundisha wanafunzi kwa kutumia teknolojia rahisi ya kusambaza elimu.
Ukuzaji wa teknolojia upo katika Mpango wa Tatu wa Maendeleo 2020/21-2025/26 ambao miongoni mwa afua za kimkakati ni pamoja na utoaji elimu bora.