Viwanda vilivyobinafsishwa havijulikana kwa majina

KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira imelieleza Bunge kuwa Viwanda vilivyobinafsishwa havijulikani kwa majina na mahali vilipo badala yake vinajulikana kwa idadi tu.
Akiwasilisha taarifa ya Kamati leo Februari Mosi, 2023 Mwenyekiti wa kamati hiyo, David Kihenzile amesema lengo la ubinafsishaji wa viwanda nchini lilikuwa kuiondolea mzigo wa bajeti Serikali, kuchangia pato la Taifa, na kuongeza wigo wa umuhimu wa Sekta Binafsi.
“Hata hivyo nia hiyo njema ya serikali haijatimia kama ilivyo kusudiwa kutokana na tija iliyopatikana kuwa ndogo, kwa mfano katika viwanda 68 kati ya 156 vilivyobinafsishwa havifanyi kazi iliyokusudiwa, viwanda 23 vinafanya kazi kwa kusuasua, viwanda 88 pekee ndivyo vinafanya kazi.” Amesema Kihenzile
Amesema, Kamati yake imebaini changamoto kwa baadhi ya viwanda vilivyo binafsishwa vimeshindwa kufanya kazi na hivyo kurudishwa tena Serikalini.
“Kwa mfano; viwanda nane vimerudishwa EPZA, viwanda vitatu vimerudishwa SIDO, NDC na Ofisi ya Rais pia serikali kukosa mapato.”Amesema
Amesema changamoto nyingine ni wananchi kupoteza ajira baada ya viwanda hivyo kufungwa au kubadilisha matumizi.
Amesema, Kamati inatambua kuwa Serikali kupitia Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu ya mwaka 2020 Ukurasa wa 58 iliahidi kuweka utaratibu wa kuendelea kufuatilia viwanda vilivyo binafsishwa ili kuhakikisha vinafanya kazi kwa malengo yaliyokusudiwa na kuongeza ajira na uzalishaji wa bidhaa nchini.
“Kamati inaamini kuwa utatuzi wa changamoto zilizobainishwa hapo juu ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi hiyo.”Amesema