Waagizwa kutoa taarifa miradi ya serikali

MAOFISA Habari serikalini wameagizwa kutangaza miradi na shughuli mbalimbali zinazofanywa na serikali ili wananchi wajue ikiwemo kujibu hoja za uongo zinazotolewa na baadhi ya watu.

Msemaji Mkuu wa Serikali, Mobhare Matinyi ametoa rai hiyo kwa halmashauri na mikoa yote nchini kuajiri maofisa habari na si watu wa Tehama ili kuhakikisha wananchi wanapata habari na miradi inayotekelezwa sehemu husika.

Akifungua mkutano wa siku tatu wa Chama cha Maofisa Mawasiliano Serikalini (TAGCO) Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk Damas Ndumbaro kwa niaba ya Naibu Waziri Mkuu,Doto Biteko amesema maofisa hao wanawajibu wakutangaza shughuli mbalimbali zinazofanywa ili watu waone ukubwa wa kazi za serikali.

Advertisement

Matinyi amesema kuwa baadhi ya halmashauri hazina maofisa mawasiliano wa serikali badala yake maofisa Tehama ndio wanaongoza kitengo hicho hali inayokwamisha hali ya wananchi kupata habari.

“Inashangaza kuona baadhi ya halmashauri kuwa na idadi ndogo ya maofisa habari huku watu wa Tehama ndio wakiongozwa idara hiyo ambao baadhi yao hawajui maana ya habari na ukiuliza sababu gani hakuna maofisa habari unajibiwa majibu yasiyorithisha.”

Kaimu Mwenyekiti wa TAGCO, Karim Meshack amesema chama hicho kitaendelea kuhakikisha kinawunganisha maofisa habari kujadili mambo mbalimbali sanjari na kujifunza mbinu mbalimbali za teknolojia za upashanaji habari.