WAANDISHI wawili kutoka Kampuni ya Magazeti ya Serikali (TSN) wameteuliwa na jopo la majaji kuwania Tuzo za Umahiri wa Uandishi wa Habari (EJAT).
Waandishi hao Vicky Kimaro na Hazla Quire watashindanishwa na wanahabari 91 kutoka vyombo vya mbali mbali vya Habari nchini katika kilele cha tuzo hizo zitakazofanyika Julai 22, 2023 katika Ukumbi wa Mlimani City.
Akitangaza wateule hao jijini Arusha leo Juni 23, 2023 Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi EJAT 2022, Kajubi Mukajanga amesema waandishi 91 wameteuliwa kati ya 728 waliowasilisha kazi zao.
Amesema kati ya hao 36 wanaandikia magazeti, 27 mitandao ya kijamii na 15 ni kutoka redioni na 15 wanatokea kwenye televisheni.
“Katika wateule wote, 44 ni wanawake ambapo 16 kutoka kwenye magazeti, 12 kutoka mitandao ya kijamii, sita kutoka katika redio na 10 ni kutoka kwenye televisheni na wanaume wote waliopenya jumla wapo 47.”Amesema Kajubi
Mgeni rasmi katika kilele cha tuzo hizo anatarajiwa kwua Jaji Othman Chande ambaye pia ni Mwenyekiti wa Tume ya Rais ya Haki Jinai.