Wabunge waifagilia TANESCO kwa ubunifu

MTWARA; KAMATI ya kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC), imeeleza kufurahishwa na ubunifu ambao umefanywa na Shirika la Umeme nchini (TANESCo) kutekeleza mradi wa kusimika mtambo wa kuzalisha umeme kutumia gesi asilia mkoani Mtwara.
Wakizungumza baada ya kukagua maendeleo ya mradi huo, wajumbe wa kamati hiyo wamesema TANESCO wametumia gharama ndogo kusimika mtambo huo, ambao unaenda kutatua changamoto kubwa ya umeme kwa Mikoa ya Lindi na Mtwara.
“Ni jambo la kuridhisha sana ukiangalia hela ambayo wametumia ni ndogo ukilinganisha na faida ya mradi, tunapongeza TANESCO kwa ubunifu huu mkubwa ambao wameonesha,” amesema Mwenyekiti wa kamati hiyo Deus Sangu .
Utekelezaji wa mradi huo wa kusimika mtambo wa kuzalisha umeme kutumia gesi asili umetokana na agizo la Rais Dk Samia Suluhu Hassan alilotoa mwezi Septamba mwaka jana kwa shirika hilo kutua changamoto ya kukatikakati umeme kwa Mikoa ya Lindi na Mtwara.
Raisi alitoa agizo hilo wakati wa ziara ya kikazi Mtwara na Lindi, ambapo alikutana na kilio cha wananchi wa mikoa hiyo wakitaka awatatulie tatizo la kukatika umeme.
Mbunge wa Kilwa Kaskazini Francis Ndulane, ameishukuru TANESCO kwa kutumia mkandarasi wa ndani kutekeleza mradi huo, huku akiitaka serikali kuendelea kutumia wakandarasi wa ndani kujenga miradi ya maendeleo.
“Najisikia faraja zaidi kuona kwamba mradi umetekelezwa ndani ya muda mfupi, umehusisha wakandarasi wa ndani wa power associate, watumishi wa TANESCO ile ahadi walitoa kwamba mtambo utawashwa mwisho wa mwezi huu, lakin siku tano kabla tunaona umeme wameshawasha, kwa kweli ni jambo la kutia moyo sana,” amesema.
Mkurungezi Mtwandaji TANESCO Gisima Nyamo-Hanga, ameimbia kamati hiyo kuwa utekelezaji wa kusimika mtambo huo ulianza Desemba mwaka jana ikiwa ni utekelezaji wa agizo la Rais.