DODOMA: WABUNGE leo Jumatatu Juni 3, 2024 wamepitisha bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa mwaka 2024/25, yenye vipaumbele 8.
Ijumaa Mei 31, 2024, Waziri wa Utalii, Angellah Kairuki aliwasilisha makadirio ya mapato na matumizi kwa wizara yake mwaka wa Fedha 2024/2025, , ambapo aliiomba iidhinishiwe Sh 348,125,419,000.
Spika wa Bunge Dk Tulia Ackson, amewapongeza Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu wa wizara na watendaji wakuu wa wizara hiyo kwa kupitishwa bajeti hiyo na kutaka wafanyie kazi maoni ya wabunge yaliyotolewa na kuwatakia kila la heri katika utekelezaji wa bajeti.
Miongoni mwa vipaumbele vya bajeti hiyo ni kuendelea kutangaza utalii ndani na nje ya nchi ikiwa ni mwendelezo wa programu maalum ya Tanzania Th e R o y al T o u r na filamu ya Amazing Tanzania.
Mikakati mingine ni kutangaza utalii kupitia matangazo katika Ligi Kuu za michezo mashuhuri duniani, matangazo kwenye ndege; misafara ya utangazaji utalii; matamasha makubwa ya kimataifa na mitandao mbalimbali ya kimataifa na vyombo vya habari.
Pia mikakati mingine ni kuibua na kuendeleza mazao ya utalii ya kimkakati ikiwemo maeneo ya malikale pamoja na utalii wa fukwe, mikutano na matukio, meli, michezo, tiba na utamaduni.