KAMATI ya kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, imeishauri serikali kuwaendeleza kielimu wataalamu wa ndani wanaosimamia na kuendesha mitambo ya kuchakata gesi asilia, ili waweze kuwa na uwezo unaotakiwa kusimamia miradi na shughuli zote zinahusu masuala ya gesi nchini.
Kamati hiyo imetoa ushauri huo mara baada ya kufanya ziara katika mitambo ya kuchakata gesi asilia eneo la Madimba, mkoani Mtwara.
Mitambo hiyo inaendeshwa na vijana wa kitanzania kupitia kampuni tanzu (GASCO) ya Shirika la Maendeleo ya Petroli Nchini (TPDC).
“Tumefurahishwa sana, kwa mfano hapa Madimba kituo hiki kinaendeshwa na Watanzania wenyewe katika mfumo mzima wa kuchakata gesi, vijana wetu wa kitanzania wasomi ndiyo wanafanya kazi hiyo,” amesema Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Dunstan Kitandula.
Amesema kuwa Kamati imeridhishwa na namna mitambo hiyo inavyoendeshwa, huku akisisitiza serikali kuendelea kuwapa elimu vijana wa kitanzania wanaosimamia, ili waweze kuwa na uwezo mkubwa wa kusimamia miradi yote na shughuli za gesi asilia kwa manufaa ya nchi.
Kampuni tanzu ya GASCO, ina wafanyakazi wa kitanzania wanaoedesha mitambo ya gesi Madimba, huku kukiwa na wafanyakazi watatu tu kutoka nje.