WASOMI na wachambuzi wa masuala ya uchumi wamempongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuunda Wizara ya Mipango na Uwekezaji.
Rais wa Chama cha Wahasibu Tanzania, Godvictor Lyimo alisema mabadiliko hayo yanaonesha kulenga kuongeza ufanisi katika kukuza uchumi.
Alisema Tume ya Mipango imekuja wakati mwafaka kwa kuwa pamoja na kuwepo mipango mingi katika kila wizara utekelezaji haukuwa na ufanisi.
Mchambuzi wa Siasa na Diplomasia, Goodluck Ng’ingo alisema uwekezaji lazima upitie hatua kadhaa kabla ya kukamilika hivyo unahitajika usimamizi.
Ng’ingo alisema wakati eneo hilo la uwekezaji lilipokuwa katika Wizara ya Viwanda na Biashara kulikuwa na mwingiliano wa sera za viwanda na biashara na hivyo kupunguza ufanisi.
Mchambuzi wa siasa na pia mhadhiri katika Chuo cha Diplomasia, Abbas Mwalimu alisema mabadiliko hayo yana umuhimu kwa kuwa diplomasia ya uchumi ilijikita zaidi kutangaza eneo la biashara na utalii na kuliacha eneo la uwekezaji.
Juzi, Rais Samia alifanya mabadiliko madogo ya miundo ya wizara na kuteua viongozi akiwamo Mbunge wa Ubungo, Profesa Kitila Mkumbo ambaye amerejeshwa kwenye uwaziri na kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji.