JESHI la Polisi Mkoa wa Pwani limewakamata watu wanne wakiwa na noti za bandia zenye thamani ya sh milioni 1.5 .
Watu hao wakazi wa Dar es Salaam walikamatwa Januari 10 mwaka huu majira ya mchana katika Kijiji cha Msata, Wilaya ya kipolisi Chalinze.
Waliokamatwa ni Zena Issa Maringa (42), Mbaraka Miraji Fundi (48), Elias Simbasi Wandiba (50) na Masumbuko Paul Kiyogoma (54).
Katika kupeleleza tukio hilo, jeshi la polisi pia lilifanikiwa kuwakamata washirika wengine wa watuhumiwa hao wakiwa na noti bandia nyingine zenye thamani ya sh milioini 12 na mtambo wa kutengeneza pesa bandia na vifaa vingine kama kompyuta, kemikali mbalimbali, gundi, jiki, tina, rangi, na bunda la karatasi zikiwa kwenye hatua za kutengeneza pesa bandia.