Wahitimu JKT Oljoro wasaidia yatima

ARUSHA; CHAMA cha Marafiki waliohitimu mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) Oljoro (MAO), mkoani Arusha wamechangishana Sh milioni 16.7 kupitia kundi lao la WhatsApp ili zisaidie shughuli za ujenzi wa eneo la kusomea na kutoa huduma ya maombi kituo cha yatima cha Habashabi, Kigongo wilayani Arusha.
Pia wametoa msaada wa vyakula,vinywaji,nguo na vitu mbalimbali kwa watoto yatima wa kituo hicho.
Akizungumza jijini Arusha, wakati wa hafla fupi ya kuwakabidhi msaada huo, Mtoa huduma kwa jamii Kanda ya Kaskazini wa MAO, Festo Msofe alisema chama hicho kilianza mwaka 2015 na 2016 walitafuta usajili baada ya kutafutana waliopata mafunzo JKT Oljoro mwaka 1991/1992 kwa lengo la kusaidiana na kusaidia jamii inayowazunguka ikiwemo yatima.
“Tuliunda group la whatsapp tukaanza kuchanga ada kila mwezi na kila mwaka tunatoa msaada kwenye eneo tunalolipendekeza, kama hapa kwenye kituo hiki tulikuja mwaka 2021 tukaona wana uhitaji wa eneo hili, tukaanza kuchangishana na leo tumetimiza ndoto yetu,” amesema.
Ameomba Watanzania kujenga utamaduni wa kuruhusu watoto wao kwenda JKT, ili kujifunza uzalendo, upendo ,kazi na tabia njema kama walivyo wao walivyojengewa tabia ya kusaidia jamii.
“Tabia ya kupenda kusaidiana tulijengewa JKT, hivyo tukipeleka watoto wetu hatutajuta, tusiwakataze kwenda JKT tutaona manufaa yake makubwa,” amesema.
Katibu wa MAO, Frida Mlingi amesema mwaka 2021 walipofika kituoni hapo kwa mara ya kwanza, walinunulia watoto bima za afya, vyakula na mwaka huu wamechangishana fedha kwa whatsApp na kuezeka eneo hilo.