Waipongeza serikali ujenzi wa majosho

WANANCHI wa Kata ya Chapakazi wilayani Kiteto,mkoani Manyara, wameelezea faida wanazopata baada ya kujengwa kwa majosho katika maeneo yao,yaliyopunguza maradhi ya mifugo na kuongeza bei ya mifugo hivyo kupata kupato kizuri.
Hayo yamebainishwa leo, katika Kijiji cha Chapakazi,wilayani Kiteto na mwakilishi wa wanakijiji hao,Justa Kalinga wakati akisoma taarifa ya ujenzi wa josho la Chapakazi mbele ya Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM),Daniel Chongolo.
Chongolo anaendelea na ziara yake mkoani Manyara ya kukagua uhai wa chama,utekelezaji wa ilani ya CCM 2020/25 na kuzungumza na makundi ya jamii.
Kalinga akisoma taarifa ya josho hilo lililogharimu zaidi ya shilingi milioni 23.7, amesema limeanza kutoa huduma kwa vitongoji vitano ambavyo ni pamoja na Msagali,Chapakazi Kati, Mnadani, Magugu na Mgombogombo.
Melchior Lameck mfugaji akizungumzia manufaa ya josho hilo eneo hilo amesema wanaishukuru serikali kwa kuwajengea majosho kwa sababu yana faida kubwa ya kupunguza magonjwa ya mifugo.
“Tunaishukuru serikali majosho haya ni faida kwetu,tumeshuhudia manufaa yake,mifugo tunaogesha kwa wiki mara mbili na chanjo tunapata mifugo haifi tena maradhi na hata ubora umeongezeka na bei ya mfugo ni nzuri kwa sasa,” amesema Lameck.
Chongolo akizungumzia josho hilo na mengine amewataka wananchi kuyatumia vizuri na kuleta mifugo yao kuogeshwa na kupata chanjo kwa sababu faida ni nyingi wanapofuata huduma na kanuni bora za ufugaji.
“Serikali inajenga majosho haya katika maeneo yote ya ufugaji nchini yatumieni kuwaletea faida, leteni mifugo iogeshwe na chanjo ipate, lakini pia mifugo ikiongezeka uzeni kiasi mpate mitaji ya kuwa na uwekezaji nwingine wa kuwaletea fedha,msifuge mifugo mingi ya kuwatesa,fugeni kulingana na eneo la malisho yaliyopo ili msilete migogoro na wakulima,”amesema Chongolo.