‘Wajibikeni kwa wakulima kuongeza uzalishaji’

MKUU wa Wilaya ya Morogoro, Rebeca Nsemwa amewataka maofisa ugani wa mkoa wa Morogoro kuwajibika kwa wakulima katika kutoa elimu ya kilimo bora, kitakachowawezesha kuongeza  tija ya uzalishaji baada ya kupatiwa nyenzo ya  usafiri wa pikipiki na serikali.

Nsemwa amesema  hayo Machi 27, 2023  kwenye hafla  ya kukabidhi pikipiki 436 kwa maofisa ugani wa mkoani Morogoro akimwakilisha Mkuu wa mkoa huo,  Fatma Mwassa.

Amesema kutokana na kuwezeshwa usafiri wa pikipiki hivi sasa, wanao uwezo kuwafikia wakulima wengi zaidi hata wale waliopo  maeneo yenye changamoto ya usafiri.

Advertisement

Amesema kwa sasa anatarajia uzalishaji kwenye sekta ya kilimo utaongezeka, kwa sababu wataweza kuwafikia wakulima kwa wakati na kutekeleza majukumu yao kwa wakati unaotakiwa.

Mkuu wa wilaya ya Morogoro, Rebeca Nsemwa ( kushoto) akijaribu kuwasha moja ya pikipiki baada ya kukabidhi Pikipiki 436 kwa maofisa ugani wa kutoka hamashauri tisa za mkoani Morogoro .(Picha zote na John Nditi).

“Tuna uhakika uzalishaji wetu maeneo yetu ya kilimo kwa sasa utakwenda kuimarika kwa sababu  wataalamu wetu  watakwenda kuwafikia au kumfikia mkulima mmoja mmoja na kumpatia elimu ya kilimo bora chenye kuleta tija, ” amesema  Nsemwa.

Mkuu wa wilaya hiyo amesema  pikipiki hizo zigawiwa kwa  maofisa hao wa kila kata kwenye kila halmashauri za mkoa wa Morogoro.

Naye  Katibu Tawala Msaidizi upande wa Uchumi na Uzalishaji , Dk Rozalia Rwegasira katika taarifa fupi kuhusiana na pikipiki hizo amesema  zimefungwa kifaa maalumu, ambacho kinaonesha mahali ambapo pikipiki hiyo ipo kwa wakati huo.

Amesema  pikipiki hizo zitawasaidia maofisa ugani kupata takwimu sahihi za wakulima katika maeneo yao, pamoja na kuwahudumia bila shida yoyote.

Add a comment

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *